TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI - NEC YAREJESHA WAGOMBEA UBUNGE 15


Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaendelea na zoezi la kupitia, kuchambua na kuzifanyia uamuzi rufaa za wagombea Ubunge zilizowasilishwa na wagombea kupitia kwa Wasimamizi mbalimbali wa Uchaguzi nchi nzima.




Kifungu cha 40(6) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, kinatoa fursa kwa wagombea wa Ubunge kukata rufaa wanapokuwa hawajaridhika na uamuzi wa Wasimamizi wa Uchaguzi kutokana na pingamizi zilizowasilishwa.

Zoezi la kuzijadili na kuzitolea uamuzi rufaa hizo linaendelea na kuanzia leo, Tume itakuwa inatoa uamuzi na kuwajulisha wahusika kwa kadri rufaa hizo zitakavyokuwa zinamalizika kushughulikiwa. Leo Tume imetoa uamuzi wa rufaa 55 za wagombea Ubunge kama ifuatavyo:

    i.Imekubali rufaa 15 na kuwarejesha wagombea katika orodha ya wagombea.

    ii. Imekataa rufaa 15 za wagombea ambao hawakuteuliwa.

    iii. Imekataa rufaa 25 za kupinga walioteuliwa.

Tume imechambua vielelezo, nyaraka na maelezo ya warufani na warufaniwa vilivyowasilishwa ili kuhakikisha kwamba haki inatendeka kwa Mujibu wa Sheria na kanuni za Uchaguzi. 

Uamuzi uliofanywa na Tume katika rufaa hizo umewarejesha baadhi ya warufani kwenye orodha ya wagombea. Tume itaendelea kutoa matokeo baada ya usajili na uchambuzi wa rufaa hizo kuanzia leo, kesho na kuendelea. 

Wahusika wa rufaa hizo wameanza kujulishwa kwa barua juu ya uamuzi wa Tume kuanzia leo. 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527