RAIS WA BELARUS ALIWEKA JESHI KATIKA TAHADHARI,MIPAKA YAFUNGWA



Belarus imesema imefunga mipaka yake na nchi za Umoja wa Ulaya. Lakini maafisa wa Poland wameielezea hatua hiyo kuwa ni "sehemu nyingine ya kampeni ya propaganda," wakisema hali ya mpakani haijabadilika



Rais wa Belarus  Alexander Lukashenko ametangaza kuwa ameliweka jeshi katika tahadhari kubwa na kufunga mipaka ya nchi hiyo na Poland na Lithuania.


Uamuzi wa Lukashenko unatilia mkazo madai yake ya kila mara kuwa wimbi la maandamano dhidi yake linachochewa na nchi za Magharibi.

 Anakabiliwa na ukosoaji kutoka kwa Marekani na Umoja wa Ulaya. Lukashenko amesema anawaondoa wanajeshi mitaani na kuwapeleka mipakani ili kuimarisha ulinzi hasa katika mpaka na Ukraine.

"Sitaki nchi yangu kuwa vitani. Isitoshe, sitaki Belarus na Poland na Lithuania kugeuka kuwa maonyesho ya kijeshi ambako masuala yetu hayatatuliwa. Kwa hivyo, leo mbele ya watu hawa wazuri kabisa, na wazalendo ninawaomba watu wa Lithuania, Poland na Ukraine - kuwakomesha wanasiasa wenu vichaa, msiruhusu vita izuke."

Maafisa wa Poland wamesema hali bado haijabadilika mpakani.


Maafisa wa mpakani wa Lithuania pia wamethibitisha kuwa hali katika mpaka na Belarus bado ni ya kawaida, wakisema wanasubiri kuona jinsi mabadiliko hayo yatavyotekelezwa.

Mapema jana, mgombea mkuu wa upinzani katika uchaguzi wa rais ambao matokeo yake yalipingwa Sviatlana Tsikhanouskaya alisema wanaharakati wanatayarisha orodha ya polisi wanaodaiwa kuhusika katika ukandamizaji dhidi ya waandamanaji.

Hapo jana, bunge la Ulaya lilipitisha kwa wingi azimio linalopinga matokeo rasmi ya uchaguzi na kusema halitamtambua Lukashenko kuwa rais halali mara baada ya muhula wake utakamilika Novemba 5.


Wizara ya mambo ya kigeni ya Urusi ilijibu ikisema wamesikitishwa kuwa Bunge la Ulaya, ambalo linajiweka kuwa mpiganiaji wa demokrasia, limeshindwa kupata nia ya kisiasa na kuangalia picha pana zaidi, na kutopendelea upande mmoja.

Credit:DW


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527