VIONGOZI WA DINI WAFURAHIA USIMAMIZI WA MIRADI YA MAENDELEO YA GGML

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel (katikati) akiwaelezea viongozi wa dini mkoani Geita mradi wa soko la dhahabu pamoja na vyumba vya biashara vilivyofadhiliwa na GGML kwa ushirikiano na Halmashauri ya Mji Geita.

Mwenyekiti wa umoja wa Dini Mkoani Geita Askofu Stephano Saguda(katikati) akimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Geita kwa kuwatembeza katika ziara hiyo na kutambua mchango mkubwa unaofanywa na Kampuni ya GGML pamoja na Serikali katika kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo Mkoani Geita.

NA MWANDISHI WETU
VIONGOZI wa dini mbalimbali mkoani Geita wamefanya ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa mkoani humo na kueleza kufurahishwa na usimamizi dhabiti miradi hiyo kwa maendeleo ya Tanzania.
Viongozi hao wamefanya ziara hiyo ambayo imedhaminiwa na Kampuniya Geita Gold Mining Limited (GGML) pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita kwa lengo la kuona na kupata ufafanuzi wa miradi inayotekelezwa mkoani humo.
Akizungumzia ziara hiyo iliyofanywa leo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel alisema ofisi yake inatambua mchango mkubwa wa viongozi wa dini katika kutunza amani na umoja ndani ya jamii.
“Huwezi kupata maendeleo katika jamii yoyote bila kuwa amani. Amani inayotupatia maendeleo katika nchi yetu na mkoa wetu wa Geita inalindwa na viongozi wa dini ambao siku zote wamekuwa na ushawishi kwa waumini wao kuhubiri amani,” alisema
Aidha, Meneja Miradi inayofadhiliwa na Geita Gold Mining Limited (GGML) kupitia fedha za Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR) Bw Moses Rusasa alisema katika ziara hiyo kuwa lengo la Kampuni ya GGML ni kuhakikisha jamii inayozunguka mgodi inafaidika.

“Tunatekeleza miradi mingi ndani ya mkoa wa Geita kwasababu mojawapo ya tunu inayoongoza Kampuniya GGML ni kufaidisha jamii inayotuzunguka. Katika ziara hii na viongozi wa dini, tumetembelea Soko la Dhahabu, Soko la Katundu pamoja na kituo cha uwekezaji (EPZA) miradi ambayo imefadhiliwa na Kampuni ya GGML kwa maendeleo ya watu wa Geita,” alisema Bw Rusasa.

Akitoa neno la shukrani wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Umoja wa Dini Mkoani Geita, Askofu Stephano Saguda alimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Geita kwa kuwatembeza katika ziara hiyo na kumpongeza kwa kazi nzuri ya kusimamia maendeleo katika Mkoa wa Geita.

“Tunampongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt John Magufuli kwa kuupatia Mkoa wa Geita kiongozi makini anayesimamia maendeleo. Nawapongeza pia Kampuni ya GGML kwa kushirikia na vyema na Serikali hususani Halmashauri za Geita na kutekeleza miradi mikubwa yenye gharama kubwa katika Mkoa wa Geita,” alisema Askofu Saguda.

Kwa miaka 10 iliyopita, GGML imewekeza Jumla ya Dola Milioni 25 kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo Mkoani Geita na Tanzania kwa ujumla. Mkakati ni kutenga pia Dola Milioni 53 kwa ajili ya miaka 14 ijayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527