WAZIRI BITEKO:ACHENI VITENDO VYA UTOROSHAJI WA MADINI

 Na.Vero Ignatus,Arusha

Waziri wa madini Doto Biteko amewataka wafanyabiashara ,wauzaji na wanunuzi wa madini Tanzania ,kufuata sheria na maelekezo mbalimbali ya serikali ,katika kufanya biashara zao, kutunza kumbukumbu,kuuza madini kwenye masoko husika,sambamba na kujiepusha na vitendo vya utoroshaji madini.

Biteko amesema kuwa Wizara ya madini imewabaini wafanyabiashara wakubwa nchini 12 wa madini ,ambao wanajihusisha na vitendo vya utoroshaji wa madini nje ya nchi,amesema wamefanya kazi ya kuwafuatilia kwa miezi 3,ambapo watoroshaji wamekuja na mbinu mpya ya kutumia magodoro,amesema serikali haitalifumbia macho jambo hilo.

''Wewe unaona kuna gari limekuja kununua magodoro Arusha,lakini wakati basi lile linaondoka au lori,unawekwa na mzigo,ambapo ule mzigo ndiyo unamaana zaidi kuliko hayo magodoro ,watanzania ni waaminifu wametupa taarifa zote ''Alisema Biteko

Amesema serikali ikimkamata mtu anatorosha madini haruhusiwi tena kufanya biashara ya madini,hivyo amesema wanapomuona mtu anatorosha madini wafahamu kuwa haibii serikali bali anawaibia watanzania kwa ujumla.

''Usalama wako wewe ni kuiangalia sheria na kuizingatia ,usipofanya hivyo utasumbuliwa hata na watu wa kawaida,utakuta mzee anasumbuliwa na katoto first apointment ,lakini kama umezingatia sheria unamwambia wewe fanya kazi yako,na bahati mbaya huko nje ya sekta watu wanaamini kuwa ninyi mnapesa nyingi tena zisizo nakazi lakini hawajui humu ndani kuna watu wanakunywa dawa za presha'' Alisema Biteko.

Amewataka wafanyabiashara hao wamadini kuhama kwenye ule utaratibu wa kununua na kuuziana, amewasisitiza kuondoka  kwenye uchuuzi na kuingia kufanya biashara ya madini,huku akiwataka kutunza kumbukumbu zao , kwani hakuna hasara ya kutunza kumbukumbu, bali ipo faida kubwa kwani zitawasaidia kwenda kwenye mabenki kwaajili ya kuombea mikopo ya kuendeshea biashara zao

Aidha Waziri Biteko amewataka TAMIDA kuchagua  viongozi wenye weledi,waso walalamishi,ambao  watawaletea mrejesho baada ya kutoka kwenye Wizara, anaweza kuwaambia ukweli hata kama wanamchukia,ambapo kupitia chama hicho kiweze kuleta wafanya biashara kutoka mataifa mengine kwaajili ya kununua madini.

Akizungumza awali mwenyekiti aliyemaliza muda wake TAMIDA Sam Mollel alimpongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kuifikisha nchi kwenye uchumi wa kati miaka mitano kabla ya 2025,udhibiti ukiwemo utoroshwaji na ulanguzi wa madini na ujenzi wa ukuta wa Mererani ,pamoja na uanzishwaji wa masoko ya serikali ya kuuzia na kununulia madini ,kwani kumeongeza mchango kwenye pato la Taifa

Amesema kuna changamoto ambazo hazijapatiwa ufumbuzi haswa ongezeko la thamani VAT ya asilimia 18% kwenye (inter-dealer trade) na majengo yanayopangishwa na wafanyabiashara wa madini,wakala wa meli Tanzania TASAC,pamoja na mlolongo wa leseni katika biashara ya usonara .

Hivyo ameuomba uongozi mpya utakaoingia madarakani baada ya uchaguzi utakuwa na kazi kubwa kuanza na TASAC ili kuwashawishi wafanyabiashara wa madini kufanya shughuli zao kwa uwazi kwa faida yao na Serikali.

Amesema kuwa TASAC ikiondolewa na kuacha kujishughulisha na sekta ndogo ya biashara ya madini itasaidia kuongeza kiwango cha usafirishaji wa madini nje ya nchi ambapo fedha za kigeni zitaongezeka nchini na kuimarisha uchumi wa nchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527