DK.HUSSEIN MWINYI AAHIDI KUENDELEZA PALE ALIPOISHIA RAIS MOHAMED SHEIN ZANZIBAR

Na Said Mwishehe,Michuzi TV
MGOMBEA Urais wa Serikali ya Mapinduzi Sanzibar kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM)Dk.Hussein Mwinyi amesema akichaguliwa kuwa Rais wa Serikali hiyo atahakikisha anafanya kazi kwa kasi kubwa ya kuendeleza pale ambapo ameishia Dk.Mohamed Ali Shein.

Dk.Hussein Mwinyi ameyasema hayo leo Agosti 29 ,2020 wakati akitoa salamu za wananchi wa Zanzibar katika uzinduzi wa kampeni za mgombea Urais wa Chama hicho Dk.John Magufuli ambapo amesema hakika Dk.Shein amefanya kazi kubwa ya kuleta maendeleo,hivyo akipata nafasi ataendeleza kuanzia pale ambapo Rais Shein ameishia.

"Zanzibar wanasema wako tayari kuwachagua viongozi wa ngazi zote katika uchaguzi mkuu mwaka huu kuanzia Rais , Wabunge, Wawakilishi,Madiwani na Viti maalum.Ilani ya CCM imetekelezwa vizuri kwa pande zote na inatoa nafasi CCM kushinda.

"Nitafanya kazi ya kuendeleza pale alipoishia Rais Dk.Shein ambaye amefanya mambo nengi na nitafanya kazi kwa kubwa sana,"amesema Dk.Hussein Mwinyi na kusisitiza kwamba atasimama imara kuleta maendeleo.

Hata hivyo amesema kwamba hakuna sababu ya kubweteka na badala yake wanachama wa CCM na mashabiki wa Chama hicho kufanya kampeni ya nguvu na hatimaye kushinda kwa kishindo na ni matumaini yake ushindi utakuwa mkubwa kuliko wakati wowote.

Wakati huo huo Dk.Hussein Mwinyi ametumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi kujiepusha na vurugu ambazo zinaweza kusababisha uvunjifu wa amani huku akifafanua tayari kuna baadhi ya watu wameanza kutoa kauli ambazo zinaonekana kuhatarisha amani ya nchi.

*Hivyo niwaombe wananchi wote tujiepushe na vurugu.Kuna wanasiasa wameanza kutoa kauli ambazo zinaashiria uvunjifu wa amani, tujiepushe na watu hao wasikuwa na nia njema na Taifa letu,"amesema Dk.Hussein Mwinyi.

Awali wakati anazungumza na wananchi waliohudhuria uzinduzi huo wa kampeni za mgombea urais wa CCM, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dk.Mohamed Ali Shein amesema kabla ya kutambulisha Dk.Hussein Mwinyi amesema Watanzania tunayo kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwani nchi yetu imepiga hatua ya maendeleo.

"Ndugu wananchi leo tunazindua kampeni yetu na mimi nimetakiwa kumtambulisha mgombea urais Zanzibar Dk.Hussein Mwinyi ambaye jina lake ni maarufu.Ni mzalendo mkubwa kwa nchi yake,ni daktari bingwa na tunaamini ataendelea kuimarisha Muungano, Umoja na mshikamano,"amesema Dk.Shein wakati anamuelezea Mgombea huyo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527