WAZIRI MKUU : TUONGEZEE BIDII ILI TUFIKIE UCHUMI WA JUU


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amewataka Watazania waendelee kufanya kazi kwa bidii ili nchi iendelee kukua kiuchumi na kufikia uchumi wa juu kwa kuwa tayari imekuwa ya uchumi wa kati.

“Kama ni mkulima lima kwa bidii, mtumishi wa umma fanya kazi kwa bidii, mlio viwandani fanyeni kazi na mamalishe nanyi pikeni sana ili mzunguko wa fedha uweze kuendelea kuwa mkubwa nchini.”

Alitoa kauli hiyo jana (Jumamosi, Julai 04, 2020) alipozindua jengo la ofisi na biashara la Mpanda Plaza lililojengwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mpanda kwa gharama ya sh bilioni  2.8.

Waziri Mkuu alisema Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani pato la mwananchi kwa mwaka lilikuwa dogo na baada ya miaka mitano limeongezeka na kufikia sh, milioni mbili.

Alisema ongezeko hilo la pato la mwananchi kwa mwaka limeliwezesha Taifa kuingia katika uchumi wa kati kabla ya matarajio yaliyopendekezwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo.

Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania ililenga kuifikisha Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati kupitia sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2025 lakini nchi imewezeka kufikia uchumi wa kati 2020.

Baada ya kuzindua jengo hilo, Waziri Mkuu alitembelea kijiji cha Kasekese kilichoko wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi ambapo alizindua msimu wa ununuzi wa zao la pamba kwa mwaka huu.

Waziri Mkuu alisema lengo la Serikali ni kurudisha ushirika  ili uweze kuwa na tija kwa wakulima, aliwataka viongozi wa Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS) wawasaidie wanachama wao.

Vilevile, Waziri Mkuu aliwaagiza Maafisa Kilimo nchini wawaelimishe viongozi wa vyama vya ushirika namna bora ya uendeshaji wa vyama hivyo ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Aliwahakikishia wananchi hao kwamba Serikali itaendelea kuwasaidia kwa kuhakikisha Maafisa Ugani wanawafikia katika maeneo yao na kuwapa elimu itakayowawezesha kujiongezea tija.

Mwisho.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527