WAZIRI JAFO AMUONDOA MENEJA WA TARURA ARUSHA KUTOKANA NA KUTOTOA TAARIFA ZA MIRADI YA MAENDELEO INAYOFANYWA NA SERIKALI

Na.Angela Msimbira ARUSHA
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Mhe. Selemani Jafo amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara za Vijijini  na Mijini Mhandisi Victor Seif kumuhamisha mara moja aliyekuwa Meneja wa Tarura Jiji la Arusha  na kumpangia kazi nyingine  ya kiwango cha chini.

Ametoa maagizo hayo jana wakati alipokuwa kwenye ziara ya kikazi ya kukagua Miradi ya maendeleo  inayotekelezwa katika Halmashauri ya Jiji la Arusha, Mkoani Arusha

Mhe. Jafo alisema ameamua kumuhamisha Mtumishi huyo kutokana na kutokutoa taarifa  za miradi ya maendeleo yanayofanywa na Serikali , jambo ambalo linasabisha  Serikali ionekane inashindwa kutimiza  majukumu yake ya kuleta maendeleo kwa wananchi

Amewaagiza watendaji  wa Halmashauri zote nchini kuhakikisha  wanasimamia miradi ya maendeleo na kutoa  taarifa kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili wananchi waweze kuijua na kutambua kuwa miradi hiyo imefanywa na Serikali

“Watendaji  wote nchini  mnawajibu wa kuhakikisha mnasimamia miradi ya Maendeleo kwa weledi mkubwa ili iweze kukamilika kwa wakati na kuitangaza kwa wananchi ili iweze kuijua, kuitunza na kuithamini miradi hiyo.” Amesisitiza Mhe. Jafo

Aidha Mhe. Jafo  amewaagiza watendaji wote nchini ambao wamepewa dhamana ya kuwahudumia wananchi watimize majukumu yao kikamilifu ili kutatua kero za wananchi kwa wakati na kuleta maendeleo kwa jamii.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527