WANACHAMA NA WAFUASI WA CHAMA CHA ACT-WAZALENDO WAMCHANGIA 500,000 MAALIM SEIF SHARIF HAMAD ILI AGOMBEE URAIS ZANZIBAR


Wanachama na Wafuasi wa Chama Cha ACT-Wazalendo wa Micheweni kisiwani Pemba wameamua kumchangia fedha Maalim Seif Sharif Hamad kuwania tena urais wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.


Akizungumza kwa niaba ya Wanachama hao ambao wamemchangia Maalim Seif kiasi cha Sh. 500,000, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Mkoa wa Micheweni kichama , Rashid Khalid amesema, wameamua kufanya hivyo kwakua kiongozi huyo ndiye pekee atakayeweza kutetea maslahi ya Wazanzibari .

Amesema kuwa, Wazanzibar wanahitaji muungano na kuwakomboa katika dimbwi la umasikini na ukosefu wa ajira ambavyo vyama vingine vimeshindwa kuwatimizia.

“Tumeamua kukuchangia fedha hizi ili zikusaidie katika kulipia ada ya uchukuaji wa fomu, sisi wanachama wa Micheweni tunaona wewe ndiye mtu pekee utakayeweza kutuokoa kutokana na madhila wanayotufanyia vyama vingine ,” amesema kiongozi huyo.

Baada ya kupokea fedha hizo, Maalim Seif amesema, kiasi hicho kitamsaidia kupunguza gharama za ada ya uchukuaji wa fomu ya kugombea urais wa Zanzibar ambayo ni shilingi milioni moja.

Pia amewashukuru wanachama hao na kusema kuwa uongozi wa Chama Cha ACT-Wazalendo kimejipanga vyema katika kuhakikisha kinapata ushindi ili kiweze kuwahudumia wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa kwa wananchi wote.

Julai 4, 2020 Maalim Seif anatarajia kuchukua fomu rasmi ya kuomba kuteuliwa na chama chake ili kugombea nafasi ya urais wa Zanzibar kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2020.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527