SIMBA SC YAITAFUNA YANGA UWANJA WA TAIFA...SASA KUKUTANA NA NAMUNGO FC FAINALI


Kiungo wa timu ya Simba, Gerson Fraga akishangilia kwa kunyoosha mikono juu baada ya kuifungia timu yake bao la kwanza.

Na Damian Masyenene -Shinyanga Press Club Blog
TIMU ya Simba SC leo imefanikiwa kusonga mbele na kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) maarufu kama Kombe la FA, baada ya kuwachapa watani wao wa jadi, Yanga SC kwa mabao 4-1 katika mchezo wa nusu fainali uliopigwa leo saa 11 jioni katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Simba wamengia kwa nguvu kubwa katika mchezo huo wakihitaji kulipiza kisasi cha kufungwa bao 1-0 katika mchezo wa ligi kuu Machi, mwaka huu, ambapo wameutawala mchezo huo wakitandika kandanda safi na kupoteza matumaini ya wapinzani wao kupata ushindi.

Mabao ya Simba yalifungwa na Gerson Fraga mnamo dakika ya 14, Cloutous Chama (49), Louis Miquissone (51) na Mzamiru Yassin (88), huku bao la kufutia machozi la Yanga likipachikwa nyavuni na Feisal Salum ‘Fei Toto’ katika dakika ya 70.

Kufuatia ushindi huo, Wekundu wa Msimbazi Simba watakutana na Namungo FC ya Lindi katika mchezo wa fainali wa michuano hiyo mwanzoni mwa mwezi Agosti, 2020 katika uwanja wa Nelson Mandela, mjini Sumbawanga mkoani Rukwa.

Namungo FC ambao ni msimu wao wa kwanza kwenye Ligi Kuu, walitinga hatua ya fainali jana Julai 11, 2020 baada ya kuwanyuka Sahare All Stars kwa bao 1-0 katika mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527