SERIKALI YAANZISHA KANDA MPYA YA WAKALA WA TAIFA WA HIFADHI YA CHAKULA (NFRA) SONGWE


Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Songwe

Serikali imetangaza kuanzisha Kanda mpya ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula-NFRA katika mkoa wa Songwe itakayohudumia mikoa ya Songwe na Mbeya.

Akizungumza na waandishi wa Habari katika eneo la Vwawa Mkoani Songwe jana tarehe 8 Julai 2020 Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga amasema kuwa Mkoa wa Songwe ulishika nafasi ya tatu Kitaifa katika uzalishaji wa mazao ya chakula nchini katika msimu wa 2018/19 hivyo Kutokana na uzalishaji huo mkubwa wa chakula, Serikali imeona ipo haja ya kuanzisha Kanda ya NFRA katika Mkoa wa Songwe, tofauti na hapo awali ambapo katika eneo la Vwawa kulikuwa na Kituo kidogo cha NFRA ambacho kilikuwa chini ya Kanda ya NFRA Makambako.

Waziri Hasunga amesema kuwa Kanda ya NFRA Songwe imeanzishwa rasmi tarehe 01 Julai, 2020 ambapo Kuanzishwa kwa Kanda hiyo kumetokana na hali ya uzalishaji mkubwa wa chakula katika Mikoa ya Songwe na Mbeya, pamoja na kujengwa kwa Maghala na Vihenge vya Kisasa ambavyo vitaongeza uwezo wa uhifadhi kutoka tani 17,000 za awali na kufikia tani 37,000.

Akizungumzia kuhusu msimu wa ununuzi wa kwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Waziri huyo Japhet Hasunga anayehudumu katika serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli akihudumia sekta ya kilimo amesema kuwa katika Kituo cha Vwawa, zoezi la ununuzi wa mahindi limeanza rasmi tarehe 06 Julai, 2020.

Ameongeza kuwa kwa sasa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula-NFRA umeanza na ununuzi wa tani 10,000 na utanunua kwa bei ya Tsh 550 kwa kilo.

Kadhalika, amesema kuwa Wakala utaendelea kuongeza kiasi cha ununuzi kadri utakavyopata fedha kutoka Serikalini. Ambapo hata hivyo amesema mtu yeyote anaruhusiwa kuuza mahindi NFRA bila kujali upendeleo wowote ilimradi mahindi hayo yawe na ubora unaotakiwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527