Picha : POLISI WAELEZA JINSI MBOWE ALIVYOVUNJWA MGUU WA KULIA....RPC AONYA WANAOTAKA KUKUSANYIKA


Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) akiwa amelazwa katika hospitali ya DCMCT iliyoko eneo la Ntyuka jijini Dodoma akiendelea kupatiwa matibabu baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana usiku wa kumakia leo nyumbani kwake jijini humo.Pichani kushoto ni Mnadhimu wa Kambi rasmi ya upinzani Bungeni (CHADEMA),Mhe, Ester Bulaya
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto, amesema kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe, amevamiwa na watu watatu waliomkanyaga na kumvunja mguu wake wa kulia.

Hayo ameyabainisha mapema leo Juni 9, 2020, na kusema kuwa taarifa kamili wataitoa hapo baadaye.

"Zipo taarifa kwamba Mhe. Mbowe amevamiwa na watu watatu, wakamkanyaga kanyaga na kumvunja mguu wake wa kulia, lakini tunafuatilia tutatoa taarifa kamili baadaye na yuko Hospitali ya Ntyuka wodi namba 4", amesema Kamanda Muroto.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema taarifa za Mbowe kushambuliwa na watu wasiojulikana walizipata asubuhi ya leo kupitia kwa Mbunge wa Viti Malum wa Chama hicho.

Muroto amesema tayari Jeshi la Polisi limeshaanza kufanya uchunguzi wa tukio hilo huku akiwaonya watu wanaosambaza taarifa za uongo pamoja na kupiga marufuku mikusanyiko yoyote isiyo halali.

"Tumepata taarifa za kuwepo kwa wanachama wa Chadema waliopanga kukusanyika kwenye ofisi za Chama cha hapa Dodoma, niwaonye kwamba Jeshi la Polisi halitoruhusu mikusanyiko kinyume na sheria na utaratibu.

Lakini pia tumelichukulia tukio hili kama tukio lingine la uhalifu na tayari tumeshaanza uchunguzi wetu, niwaonye wale wanaotaka kulitumia tukio hili kisiasa," amesema Muroto.

Taarifa zinaarifu kuwa Mbowe ameshambuliwa majira ya saa 7:00 usiku wa kuamkia leo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527