SERIKALI YAWAREJESHA WATANZANIA 119 WALIOKWAMA FALME ZA KIARABU


Takribani Watanzania 119 waliokuwa wamekwama katika nchi za Falme za Kiarabu wamerejea Tanzania na kutoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutokana na jitihada za kuwarejesha nyumbani.

Watanzania hao 119 waliokuwa wamekwama katika nchi za Falme za Kiarabu baada ya mlipuko wa ugonjwa wa COVID 19 na kusababisha mashirika mbalimbali ya ndege kufunga safari zake wamewasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere majira ya saa nane mchana kwa ndege ya shirika la ndege la Fly Dubai.

Wakizungumza wakati na  baada ya kumaliza taratibu zote za uhamiaji baadhi ya Watanzania hao ambao wengine walikuwa na watoto wadogo wamesema Maisha ya kufungiwa ndani kwa takribani miezi mitatu si rahisi hata kidogo jambo lililosababisha ugumu wa Maisha baada ya wengine akiba zao kumalizika

Kwa upande wake Bw Yahaya Abdala amesema Maisha ugenini hayakuwa rahisi baada ya kukwama kwa kuwa walishindwa kurejea Tanzania kwa mara ya kwanza kutokana na idadi ya wasafiri kuwa ndogo lakini kwa jitihada za Serikali baadae kibali cha safari kilipatikana na hatimae wamerejea Tanzania

Hii ni mara ya pili kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais John Pombe Magufuli kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuratibu na kufanikisha safari ya watanzania kurejea nyumbani baada ya kukwama ughaibuni kutokana na changamoto ya uwepo wa Virusi vya Corona na kusababisha mashirika mengi ya ndege kusitisha safari zake ambapo awali takribani watanzania 246 walirejeshwa na serikali wakitokea India na hii leo ni hawa watanzania 119 ambao walikuwa wamekwama katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527