MBUNGE AZZA HILAL ACHANGIA MIFUKO YA SARUJI KWA AJILI YA UJENZI WA UZIO SHULE YA SEKONDARI MWENDAKULIMA KAHAMA MJI



Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) amechangia Mifuko 50 ya saruji yenye thamani ya shilingi 900,000/= kwa ajili ya ujenzi wa uzio katika shule ya Sekondari Mwendakulima iliyopo katika halmashauri ya Mji Kahama.

Mhe. Azza amekabidhi mchango huo leo Jumamosi Mei 9,2020 kwa Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Anamringi Macha.

Mhe. Azza amesema mifuko hiyo ya saruji itasaidia katika ujenzi wa uzio unaoendelea katika shule ya Sekondari Mwendakulima ambayo wasichana wanakaa bweni ili kusaidia kuimarisha ulinzi katika shule hiyo.

“Tukiwa kwenye ziara ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwenye shule hiyo mwaka 2018 katika risala yao walieleza changamoto ya kutokuwa na uzio nikaahidi kuwa na mimi nitachangia ili watoto wetu wasome katika mazingira bora na salama zaidi”,ameeleza Mhe. Azza.

“Mhe. Mkuu wa wilaya nimenunua mifuko 50 ya saruji yenye thamani ya shilingi 900,000/=, naomba kukukabidhi risti ya manunuzi ya mifuko hiyo ya saruji ambayo itapelekwa shuleni”,ameongeza.

Mkuu wa wilaya ya Kahama, Mhe. Anamringi Macha alimpongeza Mhe. Azza kuendelea kutekeleza ahadi alizoziahidi kwa wananchi na kueleza kuwa mifuko hiyo ya saruji itatumika kwa malengo yaliyokusudiwa kuboresha miundombinu ya shule ya Sekondari Mwendakulima.

“Mhe. Azza ni Mbunge anayetekeleza kwa vitendo ahadi alizoahidi na wakati wa uchaguzi aliomba ushirikiano na ameouonesha katika kuwaletea maendeleo wananchi,tunamshukuru sana kwa mchango wake na siyo mara yake ya kwanza kufika Kahama kuchangia shughuli za maendeleo…huu ni mwendelezo wa shughuli ambazo amekuwa akizifanya”,ameongeza Macha.

Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wananchi kuendelea na shughuli zao za kila siku huku wakichukua tahadhari dhidi ya Ugonjwa wa Corona.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Anamringi Macha risti ya manunuzi ya Mifuko 50 ya saruji yenye thamani ya shilingi 900,000/= kwa ajili ya ujenzi wa uzio katika shule ya Sekondari Mwendakulima iliyopo katika halmashauri ya Mji Kahama. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Anamringi Macha akimshukuru Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) kwa mchango wa mifuko 50 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa uzio katika shule ya sekondari Mwendakulima.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527