SHIRIKA LA MEDO LA MKOANI SINGIDA LATOA ELIMU YA KUJIKINGA NA CORONA



Daktari Mgonza Mgonza (kushoto) kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Wilaya ya Singida, akiwaelekeza wananchi namna  sahihi ya kuvaa na kuvua barakoa katika kampeni ya utoaji elimu ya kujikinga na ugonjwa wa Corona Wilaya ya Singida.
 Afisa Miradi wa  Shirika la Mtinko Education Development Organization (MEDO),  Hasan Rasuli akiwaelekeza wananchi jinsi ya kusafisha mikono kwa usahihi.




 Mohamed Mpera kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Wilaya ya Singida, akiwaelekeza wananchi namna  sahihi ya kunawa mikono.



 Hii ni miongoni mwa ndoo chache  zilizopo katika Soko la Njia Panda wilayani Singida, lakini haina sabuni.


 Elikarim Sima (kulia) kutoka Shirika la MEDO, akiwaelekeza wananchi namna  sahihi ya kunawa mikono.
Dkt. Rachel Enock, akielekeza wananchi barakoa mbadala zinazokinga Virusi vya Corona. 



Na Boniphace Jilili, Singida.

HALMASHAURI ya Wilaya ya Singida Mkoani Singida kwa kushirikiana na Mashirika yasio ya Kiserikali ya Mtinko Education Development Organization (MEDO) pamoja na Action Aid Tanzania yametoa elimu ya kujikinga na Corona kwa wananchi wa Halmashauri hiyo.

Ofisa miradi kutoka Shirika la Mtinko Education Development Organization (MEDO) Hassan Rasuli amesema wanatekeleza kazi hiyo ya utoaji elimu ya kujikinga na ugonjwa wa Corona kwa wananchi wa Halmashauri ya Singida chini ya Mradi wao wa "Haki kodi, huduma za jamii zinazozingatia mahitaji ya kijinsia na kuvunja vikwazo"kwa ushirikiano wa Mkurugenzi wa Halmashauri na Action Aid.

Rasuli amesema lengo la utoaji wa elimu hiyo ni kuhakikisha wananchi wanakuwa na uelewa wa kutosha wa maelekezo yanayotolewa na wataalamu wa afya ikiwemo kunawa mikono kwa usahihi mara kwa mara tena kwa maji tiririka na sabuni pamoja na kuvaa barakoa ili kuendelea kujikinga na maambikizi ya virusi vya Covid-19. 

kaimu mganga Mkuu Wilaya hiyo Mgonza S Mgonza amesema wameelekeza wananchi namna ya kuchukua tahadhari ili kujikinga na ugonjwa wa Corona ikizingatiwa maeneo mengi ya Wilaya hiyo ni vijijini.

"Safisha mikono yako mara kwa mara kwa maji tiririka kwa kutumia sabuni au dawa ya kutakasa mikono na baada ya kunawa epuka kugusa macho,pua au mdomo na nguo badala yake jifute kwa kutumia tishu ambayo itatupwa sehemu salama baada ya kutumika."alisema Mgonza.

Aidha Ofisa miradi kutoka MEDO alisema wananchi wengi hawazingatii maelekezo yanayotolewa na wizara ya afya licha ya maeneo mengi yanayotoa huduma mbalimbali za kijamii kuwa na vifaa vya kunawia mikono.

"Tumepita kwenye maduka mengi wenye maduka wameweka ndoo za kunawia lakini hazina sabuni,licha ya kuweka ndoo hizo wananchi pia wengi hawanawi." alisema Rasuli.

Katika elimu hiyo ambayo imetolewa kwenye kata zote za Wilaya hiyo kwa nyakati tofauti ndani ya siku tano kwa kutembelea maeneo ya minada, maduka,magulio na maeneo mengine yaliyoonekana kukusanya watu itakuwa ni sehemu ambayo imewakumbusha wananchi kuwa ugonjwa wa Corona upo hivyo waendelee kuchukua tahadhari. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527