MADEREVA WA TANZANIA WALALAMIKA ZOEZI LA UPIMAJI CORONA MPAKA WA NAMANGA KWENDA KENYA

Madereva wa malori na magari 302 waliokuwa wanasafirisha bidhaa na abiria kwenda nchi jirani ya Kenya, jana walizuiliwa katika mpaka wa Namanga hivyo kushindwa kuingia nchini Kenya hadi hapo watakapopimwa kama wana virusi vya Corona na kusubiri majibu ndani ya masaa 48.

Wakizungumza katika mkutano ulioitishwa na mkuu wa wilaya ya Longido, Frank Mwaisumbe, baadhi ya madereva hao, walilalamikia zoezi hilo la upimaji wa nguvu mpakani na huku wakihofia pia matokeo ya vipimo.

Dereva Audax Ntebe amesema wamekosa Imani na zoezi la upimaji kwa kuwa hakuna tahadhari ya upimaji lakini pia hakuna uwakilishi wa Tanzania huku dereva Kassim Mkali akisema wakati wamezuiwa kuingia kenya, bado wanalipishwa ushuru wa maegesho kwa siku kiasi cha sh 4000 na fedha za ulinzi wa magari sh 3000 kwa siku jambo ambalo linaendelea kuwapa ugumu wa maisha.

Akizungumza na madereva hao, mkuu huyo wa wilaya, Mwaisumbe alisema tayari amewasiliana na mkuu wa wilaya ya Kajiado juu ya kupinga zoezi hilo ambalo amesema haliendi katika hali sahihi kutokana na kukosa uwakilishi kwa upande wa Tanzania.

Kufuatia hatua hiyo Mwaisumbe amesema kuanzia sasa magari na madereva kutoka kenya wanaoingia nchini, pia watatakiwa kupimwa na kusubiri majibu masaa 48 kama wanavyofanya wakenya.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527