DEOGRATIUS NSOKOLO ACHAGULIWA TENA KUWA MWENYEKITI WA CHAMA CHA WAANDISHI WA HABARI KIGOMA..VIONGOZI WENGINE HAWA HAPA

Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari wa Mkoa wa Kigoma (KGPC)Deogratias Nsokolo akishukuru wajumbe wa mkutano mkuu kwa kumpa fursa ya kuongoza chama hicho kwa kipindi cha miaka mitano.
Wajumbe wa mkutano mkuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na uongozi mpya wa Kigoma Press Club(KGPC) waliouchagua
Na Editha Karlo,Kigoma
Wanachama wa Chama cha Waandishi wa habari wa Mkoa wa Kigoma (Kigoma Press Club - KGPC) wamewachagua viongozi wapya wa chama hicho katika nafasi mbalimbali ambao wataongoza kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka huu 2020 hadi mwaka 2025.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi uliofanyika Jumamosi Mei 16,2020 katika ukumbi wa ofisi za KGPC Mwenyekiti wa uchaguzi huo Richard Katunka ambaye ni Mwandishi wa Star tv Mkoani Kigoma alisema Mwenyekiti mpya wa chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Kigoma ni Deogratius Nsokolo,huku nafasi ya makamu Mwenyekiti ikichukuliwa na Jacob Ruvilo.

Amesema wanachama wamemchagua Deogratis Nsokolo kwa kura wajumbe wote 28 kumpigia kura za ndiyo kuwa mwenyekiti mpya ambayo ni nafasi yake aliyokuwa anaitetea.

Nsokolo ambaye ni mwandishi wa ITV Mkoa wa Kigoma pia Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari nchini Tanzania (UTPC) aligombea nafasi hiyo ya Mwenyekiti akiwa hana mpinzani hivyo wajumbe walimpigia kura za ndiyo na hapana na kufanikiwa kunyakua kura zote za ndiyo.

Nafasi ya makamu mwenyekiti imenyakuliwa na Jacob Ruvilo mwakilishi wa Azam Tv Mkoa wa Kigoma aliyeshinda kwa kura 22 za ndiyo ambapo nafasi hiyo alikuwa anaiwania peke yake.

Nafasi ya katibu Mkuu wa KGPC ilichukuliwa na Mwajabu Hoza mwakilishi wa Channel Ten Mkoa wa Kigoma baada ya kupata kura 15 na kumshinda mpinzani wake Fadhil Abdallah mwandishi wa Magazeti ya TSN aliyekuwa akitetea nafasi yake aliyepata kura 9  huku Rhoda Ezekiel mwandishi wa gazeti la Uhuru alijitoa kwenye nafasi ya kugombea ukatibu na nafasi ya katibu msaidizi ikichukuliwa na Emanuel Senny mtangazaji wa radio Joy aliyepata kura 22.

Nafasi ya Mweka hazina ilichukuliwa na Winne Bwire kwa kupigiwa kura za ndiyo 27 kati ya kura 28.

Kwa upande wa wajumbe wa kamati tendaji waliochaguliwa ni Prosper Kwigize mwakilishi wa DW aliyepata kura 14 Happy Tesha mwandishi wa gazeti la Mwananchi kura 15  na Adrian Eustate mtangazaji wa radio Kwizera aliyepata kura 23 jumla ya wagombea sita walijitokeza kugombea nafasi hizo.

Akizungumza baada ya uchaguzi Mwenyekiti mpya Deogratias Nsokolo aliwapongeza wajumbe kwa kumchagua na kuendelea kuwa na imani naye kuendelea kuongoza KGPC kama mwenyekiti aliahidi ushirikiano ili kuendeleza Klabu hiyo na kuwataka wanachama kutoa ushirikiano kwa uongozi huo mpya.

Aliwataka pia wanahabari kuchukua tahadhari wanapokuwa katika majukumu yao ya kazi kutokana na janga hili lililopo sasa la virusi vya Corona

"Wakati tulionao sasa ni wakati wa hatari kwa sababu ya ugonjwa huu wa virusi vya Corona na kazi zetu hizi kuna kipindi inatulazimu kujitumbukiza kwenye mikusanyiko mikubwa ya watu tuwe na tahadhari ugonjwa huu hautahangalia eti wewe ni mwandishi tuchukue tahadhari kama tunavyoshauriwa na wataalam wa afya juu ya ugonjwa huu",alisema Nsokolo

Pia aliwataka waandishi kutumia kalamu zao kuelimisha jamii namna ya kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa huo kwa kufuata maelekezo ya wataalam wa afya.

Naye mwanachama Antony Kayanda amewataka viongozi hao wapya kuendeleza yale mazuri yote yaliyofanywa na uongozi uliopita ili kuendeleza Klabu hiyo ambayo imekuwa mfano kwa Klabu zingine nchini.

Naye mwanachama Magreth Magosso Abdallah amewapongeza viongozi wote waliochaguliwa katika nafasi mbalimbali na kuwataka kuendeleza yale mazuri yote yaliyoanza kufanywa na viongozi waliomaliza muda wao.

"Nina wapongeza nyote mlioshinda na kutangazwa na mlioshinda lakini kura hazikutosha nawapongeza pia tusonge mbele tuijenge KGPC yetu nguvu yetu inatosha kukipeleka chama chetu mbele",alisema

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527