BURUNDI YAWATIMUA NCHINI HUMO MAAFISA WA SHIRIKA LA AFYA DUNIANI (WHO)


Serikali ya Burundi imemfukuza nchini humo Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini humo na maafisa watatu wa timu yake waliokuwa wakifuatilia mwenendo wa mlipuko wa ugonjwa wa Covid-19 (corona) katika nchi hiyo.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Burundi imeiandikia barua ofisi kuu ya WHO barani Afrika, ikitaka iwaondoe maafisa wake hao nchini humo kufikia leo Ijumaa.

Maafisa hao wa WHO waliotimuliwa ni pamoja na Mwakilishi Mkazi wa WHO nchini Burundi, Dakta Walter Kazadi Mulombo, Dakta Jean Pierre Mulunda Nkata, mshirikishi wa mlipuko wa corona wa WHO, Dakta Ruhana Mirindi Bisimwa, Mkuu wa Magonjwa ya Kuambukiza na Profesa Daniel Tarzy, mtaalamu wa maabara ya kupima virusi vya corona wa shirika hilo la afya duniani.

Afisa mmoja wa Wizara ya Afya ya Burundi ambaye hakutaka kutaja jina lake ameliambia shirika la habari la AFP kuwa, maafisa hao wa WHO wametimuliwa kwa kukosoa namna wizara hiyo inavyolishughulikia janga la corona.

WHO na CDC-Afrika zilitaka kupinga kuendelea kufanyika mikutano ya kampeni za uchaguzi mkuu ujao nchini humo kisa Corona.

Kwa mujibu wa takwimu za serikali, nchi hiyo yenye watu milioni 11 imerekodi kesi 27 tu za watu walioambukizwa virusi vya corona hadi sasa, huku mtu mmoja akiaga dunia

Uchaguzi wa urais, bunge na madiwani nchini Burundi unatazamiwa kufanyika tarehe 20 ya mwezi huu wa Mei.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527