Picha : SHUWASA YATOA MSAADA WA NDOO 15 ZENYE UJAZO WA LITA 45 KUKABILIANA NA CORONA KATIKA MANISPAA YA SHINYANGA



Mkurugenzi wa SHUWASA Bi. Flaviana Kifizi (kulia) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (kushoto) ndoo 15 zenye ujazo wa lita 45 kila moja kwa ajili ya kunawia mikono katika maeneo ya huduma za kijamii ili kukabiliana maambukizi ya Virusi vya Corona (Covid -19) 



Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog  
Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) imetoa msaada wa ndoo 15 zenye ujazo wa lita 45 kwa ajili ya kutumika kunawia mikono katika maeneo ya huduma za kijamii ili kusaidia katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona (Covid -19) katika Manispaa ya Shinyanga.

Ndoo hizo zimekabidhiwa leo Jumanne Aprili 21,2020 na Mkurugenzi wa SHUWASA Bi. Flaviana Kifizi kwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko ambaye pia amemkabidhi Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Geofrey Mwangulumbi kwa ajili ya kuzisambaza katika maeneo yenye huduma za kijamii.

Akikabidhi ndoo hizo, Kifizi alisema SHUWASA inaunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali katika kukabiliana na Maambukizi ya Virusi vya Corona na wananchi wahakikishe wananawa mikono kwa maji tiririka na sabuni.

“Tumezunguka katika maeneo mbalimbali katika Manispaa ya Shinyanga na kubaini kuwa baadhi ya maeneo yenye huduma za kijamii mfano sokoni wananchi wanatumia ndoo ndogo na chache kunawia mikono yao ndiyo maana tumeona ni vyema nasi tuchangie kwa awamu ya kwanza ndoo hizi 15 zenye ujazo wa lita 45 kila moja”,alisema Kifizi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko aliishukuru SHUWASA kwa mchango huo wa ndoo za kunawia mikono huku akiwaomba wadau wengine kujitokeza kushirikiana na serikali katika kukabiliana na ugonjwa wa Corona kwani ni jukumu la kila mwananchi kuhakikisha maambukizi ya Virusi vya Corona havisambai katika jamii.

“Kwa niaba ya uongozi wa serikali niwashukuru sana SHUWASA kwa mchango huu ambao unaongeza juhudi za  katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona. Tutazisambaza ndoo hizi katika maeneo yenye huduma za kijamii ikiwemo kwenye masoko ili kupunguza foleni lakini pia kuimarisha zaidi usafi”,alisema Mboneko.

“Naomba tuendelee kuhamasisha wananchi kunawa mikono kwa maji na sabuni kabla ya kupata huduma za kijamii katika maeneo mbalimbali ikiwemo masoko na vituo vya mabasi na kuhakikisha maji yanakuwepo kila wakati”,aliongeza Mboneko.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wazazi,walezi na jamii kuwazuia watoto wasizulule mtaani badala yake watulie majumbani ili kuwaepusha wasipate maambukizi ya Virusi vya Corona.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Geofrey Mwangulumbi alisema atahakikisha maji ya kunawa yanakuwepo kila wakati na kwamba wataweka askari wa Jeshi la Akiba ‘Mgambo’ katika maeneo ya huduma za kijamii ili kusimamia zoezi la kunawa mikono kwa kila mtu anayefika katika maeneo hayo.

ANGALIA PICHA
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) Bi. Flaviana Kifizi (kulia) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (kushoto) ndoo 15 zenye ujazo wa lita 45 kila moja kwa ajili ya kunawia mikono katika maeneo ya huduma za kijamii ili kukabiliana maambukizi ya Virusi vya Corona (Covid -19) leo Jumanne Aprili 21,2020. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) Bi. Flaviana Kifizi akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (kushoto) ndoo 15 kwa ajili ya kunawia katika maeneo ya huduma za kijamii kukabiliana na ugonjwa wa Corona. Wa Kwanza kushoto ni Katibu Tawala Wilaya ya Shinyanga, Boniface Chambi,wa kwanza kulia ni Afisa Mahusiano wa SHUWASA, Bi. Nsianel Gelard,wengine ni wafanyakazi wa SHUWASA.
Ndoo 15 zenye ujazo wa lita 45 zilitolewa na SHUWASA kwa ajili ya kunawia katika maeneo ya huduma za kijamii kukabiliana na ugonjwa wa Corona katika wilaya ya Shinyanga.
Kulia ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA)  Bi. Flaviana Kifizi akimwelezea Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko lengo la SHUWASA kuchangia ndoo za kunawia mikono katika maeneo ya huduma za kijamii.
Kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akiwashukuru viongozi wa SHUWASA kuchangia ndoo za kunawia mikono katika maeneo ya huduma za kijamii.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akisisitiza umuhimu wa kuhamasisha kila mwananchi anayefika katika maeneo ya huduma za kijamii ananawa mikono kwa maji safi na sabuni ili kukabiliana na maambukizi ya Virusi vya Corona.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akipiga picha ya kumbukumbu na viongozi wa SHUWASA baada ya kupokea ndoo 15 zilizotolewa na SHUWASA kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya Virusi vya Corona katika maeneo ya huduma za kijamii.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko  (katikati) akiomuonesha Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Geofrey Mwangulumbi ( wa pili kushoto) ndoo zilizotolewa na SHUWASA kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya Virusi vya Corona katika maeneo ya huduma za kijamii.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko  (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Geofrey Mwangulumbi  ndoo zilizotolewa na SHUWASA kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya Virusi vya Corona katika maeneo ya huduma za kijamii.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Geofrey Mwangulumbi (wa pili kushoto) akizungumza baada ya kukabidhiwa na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko ndoo 15 zilizotolewa na SHUWASA kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya Virusi vya Corona katika maeneo ya huduma za kijamii.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527