KIJANA ANUSURIKA KUFA KWA KUKATWA WEMBE SEHEMU ZA SIRI NA MPENZI WAKE SHINYANGA


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kijana aliyejulikana kwa jina la Shaibu Hamis mkazi wa Mtaa wa Mabambasi kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga anayefanya kazi ya kuzoa taka amenusurika kufa baada ya kukatwa viwembe sehemu zake za siri na mpenzi wake katika mzozo wa fedha baada ya kutoka katika Kilabu cha Pombe za Kienyeji maarufu ‘Kahama Kilabu’ iliyopo eneo la Tambukareli Mjini Shinyanga. 


Akizungumza na Malunde 1 blog, Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Mabambasi Bakari Hamis amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Jumanne Aprili 7,2020 majira ya saa saba usiku. 

Inaelezwa kuwa chanzo cha tukio hilo ni ugomvi kati ya wapenzi hao wawili uliotokana na Pesa/posho ya Shaibu aliyopokea kutoka Kampuni ya Wakala wa Kuzoa Taka mjini Shinyanga ‘Mpungwa Investment’ anakofanyia kazi ambapo mwanamke huyo alikuwa anazitaka hizo pesa na katika purukushani hizo mwanamke huyo akamkata wembe mpenzi wake kwenye sehemu za siri. 

Mwenyekiti huyo wa mtaa amesema tukio hilo lilitokea baada ya Shaibu na mpenzi wake ambaye hajajulikana jina lake kutoka kwenye starehe zao katika Kilabu cha Pombe za Kienyeji inayojulikana kwa jina la Kahama Kilabu. 

“Shaibu alikuwa na mpenzi wake ambaye anadaiwa kuwa naye kwenye mahusiano ya kimapenzi kwa takribani wiki moja sasa walitokea kwenye starehe zao katika klabu ya pombe za kienyeji Kahama Kilabu iliyopo relini hapo. Wanajua wao walikuwa wanafanya nini huko Kilabu lakini walikunywa wote pombe wakarudi nyumbani wakaingia kulala,sasa kilichotendeka kule Kilabuni na ndani ya nyumba yao wanajua wao”,anasimulia Bakari Hamis. 

“Mimi wamekuja kwangu kuniamsha majira ya saa saba usiku, akaja mjeruhiwa na majirani waliomsindikiza nikawapa barua ya kwenda polisi na walipofika huko polisi wakapewa fomu ya kwenda hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya matibabu.Madaktari walivyomfanyia uchunguzi wao wakaona ni dalili ya kukatwa viwembe akashonwa nyuzi sita”, ameongeza.

Amesema Shaibu alipatiwa matibabu na kuruhusiwa kutoka na sasa anaendelea vizuri.

“Chanzo huenda ni ulevi,kwani ulevi ule wa kunywa bila mipaka unasababisha maafa ulevi unatakiwa unywe kama burudani kidogo unarudi nyumbani lakini ule ulevi wa kunywa mpaka unashindwa kujitambua ni hatari”,amesema Mwenyekiti wa mtaa. 

“Mwanamke inasemekana ni mkazi wa mtaa wa Dome bado sijapata jina lake maana kwa jinsi walivyokuja usiku ule walionekana pombe zipo kichwani. Kesi imeshafika polisi ni wajibu wao kumkamata",amesema mwenyekiti huyo wa mtaa. 

Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga ACP Debora Magiligimba amesema hajapata taarifa kuhusu tukio hilo na kuahidi kufuatilia kwa taarifa zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527