MAENDELEO YA UBUNIFU WA MJI WA SERIKALI YAJADILIWA


Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea na zoezi la kuratibu awamu ya pili ya uendelezaji wa mji wa serikali eneo la Mtumba, makao makuu ya nchi jijini Dodoma. Awamu hii ya pili inahusisha Ubunifu na ujenzi wa majengo makubwa ya Ofisi zitakazotumiwa na Wizara za serikali.

Akiongea, tarehe 20 Aprili, 2020,  katika kikao cha Kamati ya Makatibu wakuu na Wataalamu wa michoro ya Ubunifu na usanifu , Katibu Mkuu ofisi ya Waziri Mkuu, (Waziri Mkuu na Bunge), Tixon Nzunda, amefafanua kuwa awamu hii ya pili ya mpango huo inajikita katika kuboresha ubunifu na usanifu wa mji wa serikali, ulioko Mtumba, Jijini Dodoma.

Aidha, kufanikiwa kwa  mpango huo ni kutachangiza jiji la  Dodoma kuwa jiji bora na la kisasa linaloendana na mahitaji na mifumo ya majiji bora duniani. Ili kufikia azma hiyo, tayari Timu ya Wataalam  imepitia michoro ya ubunifu na usanifu. Pia Wakala wa majengo Tanzania (TBA), inaendelea kufanya kazi kwa karibu na  Taasisi nyingine zinazohusika na miundo mbinu katika mji wa Serikali kama vile TARURA, DOWASA, TANESCO, ZIMAMOTO, TPDC, TTCL na eGA.

Hivi karibuni , Mwezi Februari mwaka huu, 2020, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa alizindua Mpango Kabambe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ambapo aliwataka wadau mbalimbali kutoa ushirikiano kwa kiwango cha juu katika utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kulifanya kuwa jiji bora na la kisasa nchini.

Serikali, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kutekeleza zoezi la kuhamishia shughuli za Serikali Kuu Dodoma. Tangu utekelezaji wa zoezi hilo uanze mwezi Septemba 2016.

Uamuzi wa kuhamishia shughuli za Serikali Dodoma ulifanyika mwaka 1973 ikiwa ni maelekezo ya Chama cha TANU kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa utawala wa awamu ya kwanza chini ya Uongozi wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

MWISHO.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527