JBS FUEL COMPANY YATOA MSAADA KWA WATOTO WENYE UALBINO BUSEGA KUKABILI CORONA

Na Stella Kalinga, Simiyu RS

Mkurugenzi wa Kampuni ya JBS Fuel Company Limited ya Mjini Bariadi, Bi. Lucy Sabu ametoa msaada chakula na vifaa mbalimbali vya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona, katika kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu cha Bikira Maria kilichopo Lamadi wilayani Busega.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo Bi. Sabu  amevitaja vifaa hivyo kuwa ni pamoja na Vitakasa mikono, sabuni za maji, ndoo kwa ajili ya maji ya kunawia mikono, mahindi na sukari vyote vikiwa na thamani ya shilingi milioni mbili (2,000,000/=).

Amesema wito uliotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli wa maombi ya siku ya tatu umemsukuma kutoa msaada huo kwani ameona ipo haja ya kuwasaidia wahitaji katika kipindi hiki cha Janga la Corona na kutoa wito kwa Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari na kufuata maelekezo ya wataalam wa afya.

"Namshukuru sana Mhe. Rais kwa maono yake kwa Watanzania kufanya maombi ya siku tatu kumuomba Mungu atuepushe na Janga la Corona, maombi haya yamenikumbusha kuwakirimu wahitaji na ndiyo maana nimeguswa kufika katika kituo hiki; nitoe wito kwa Watanzania wote kuwakumbuka wahitaji katika kipindi hiki cha Janga la Corona," alisema Bi Lucy Sabu.

Akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka, Mkuu wa Wilaya ya Busega Mhe. Tano Mwera amemshukuru Bi. Lucy Sabu kwa namna alivyoguswa kusaidia kituo hicho huku akiendelea kusisitiza wananchi kuchukua tahadhari na kumwelekeza Mkurugenzi wa kituo kuwa makini kudhibiti watu wanaoingia kituoni hapo ili kuwalinda watoto.

Naye Mratibu wa mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona Mkoani Simiyu, Dkt. Khamis Kulemba ameutaka Uongozi wa kituo hicho kuongeza maeneo ya watoto kunawa mikono pamoja na kuwasisitiza kunawa mara kwa mara.

Mkurugenzi wa kituo cha Bikira Maria, Sister Helena Ntambulwa amemshukuru Bi. Lucy Sabu kwa msaada aliotoa na kuwashukuru viongozi wa Wilaya ya Busega na Mkoa wa Simiyu kwa namna wanavyokisaidia kituo hicho chenye jumla ya watoto 71 ambao wanatoka maeneo  mbalimbali ya Tanzania wakiwemo waliopoteza wazazi na waliotelekezwa.

Kwa upande wake Mjumbe wa Bodi ya wadhamini ya Kituo hicho, Bw. Belensi China amesema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwa ni pamoja na upungufu wa fedha za kulipa matibabu ya watoto na mishahara ya wafanyakazi; hivyo amewaomba Watanzania wenye mapenzi mema kuendelea kuwasaidia watoto hao wenye mahitaji maalum.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527