WAVUVI WADOGO WACHANGIA MAPATO MAKUBWA SEKTA YA UVUVI NCHINI



Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Magese Bulayi,akizungumza wakati akifungua Warsha ya Kuwajengea Uelewa Watalaamu wa Uvuvi kuhusu Mwongozo wa Hiari wa kuhakikisha Uvuvi Mdogo unakuwa endelevu nchini iliyofanyika jijini Dodoma.
Sehemu ya washiriki wakifuatilia hotuba ya Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Magese Bulayi, wakati akifungua Warsha ya Kuwajengea Uelewa Watalaamu wa Uvuvi kuhusu Mwongozo wa Hiari wa kuhakikisha Uvuvi Mdogo unakuwa endelevu nchini iliyofanyika jijini Dodoma.
Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Magese Bulayi,akiwa katika picha ya pamoja na washiriki mara baada ya kufungua Warsha ya Kuwajengea Uelewa Watalaamu wa Uvuvi kuhusu Mwongozo wa Hiari wa kuhakikisha Uvuvi Mdogo unakuwa endelevu nchini iliyofanyika jijini Dodoma.

............................................................

Na.Alex Sonna,Dodoma

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Uvuvi), Magese Bulayi,amesema kuwa asilimia 95 ya mapato yanayopatikana kwenye Uvuvi wa mazao ya Samaki katika bahari,maziwa,mabwawa na mito kwa mwaka huchangiwa na wavuvi wadodo nchini.

Hayo ameyasema leo jijini Dodoma wakati akifungua Warsha ya Kuwajengea Uelewa Watalaamu wa Uvuvi kuhusu Mwongozo wa Hiari wa kuhakikisha Uvuvi Mdogo unakuwa endelevu nchini.

Bw.Bulayi amewataka watalaamu hao kutoa maoni yao kwa uhuru yatakayosaidia kuandaa Mpango wa Utekelezaji wa Mwongozo wa hiari kuhakikisha uvuvi mdogo unakuwa endelevu nchini.

Hata hivyo amesema kuwa sekta ya uvuvi kote duniani kama vile nchini ni muhimu sana, kulingana na takwimu za Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) watu milioni 120 duniani wanajishughulisha na shughuli za uvuvi.

“Kati ya asilimia 90 wameajiriwa au kujiajiri katika uvuvi mdogo, ambapo kati ya hao, asilimia 50 ni akinamama,” alisema.

Aidha Bulayi amesema kuwa asilimia 90 ya watu waliopo katika uvuvi mdogo wamo katika nchi zinazoendelea na hivyo kiwezesha asilimia 95 ya samaki wanaovuliwa na wavuvi wadogo kitumiwa katika nchi zinazoendelea na hatua hii itasaidia sana kuhakikisha usalama wa chakula katika nchi zetu.

Bulayi amesema kuwa katika hali ya kushangaza katika kundi hilo la wavuvi wadogo watu milioni 5.8 wanaishi kwa kipato cha chini ya wastani wa dola moja ya kimarekani kwa siku ambayo ni sawa na sh 2,200 za kitanzania.

Amesema kuwa si jambo jema kujisifia kwamba tuna rasmali nyingi za uvuvi na zenye thamani kubwa, wakati watu wanaoshiriki shughuli za uvuvi wamo katika lindi la umasikini mkubwa.

Hata hivyo amesema amesema kuwa Serikali imekuwa ikijitahidi sana kutatua changamoto wanazokumbana nazo wavuvi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji na mikopo, matumizi ya teknolojia duni, upotevu wa mazao yaliyovunwa na ugumu wa kuyafikia masoko.

"Hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kusaidia kutatua changamoto hizo ni pamoja na kuandaa Sera ya uvuvi, sheria, kanuni na miongozo mbalimbali ya mpango kabambe wa kuendeleza sekta ya Uvuvi."

Naye mwenyekiti wa kikosi kazi cha Taifa cha kutekeleza mwongozo wa hiari wa kuendeleza uvuvi mdogo, Bw. Yahya Mgawe amesema kuwa Serikali imeweka mfumo wa huduma za ugani ambazo zinatolewa katika Halmashauri karibu zote nchini, hii ni pamoja na huduma za utoaji mafunzo ya uvuvi na ufugaji samaki ambayo yanatolewa sehemu mbalimbali nchini.

"Pamoja na juhudi zetu zote hizi, hali ya wavuvi wadogo bado haijafikia matamanio ya Serikali, kipato chao, vyombo wanavyotumia, mitego wanayotumia ni duni na hawawezi kwenda kwenye maeneo ambayo yana samaki wengi." Amesema Mgawe.

Kwa upande wake Mwakilishi wa FAO, Dk Oliver Mkumbo ameishukuru Serikali kwa kuandaa warsha hii ya kujenga uelewa na kukusanya maoni yatakayosaidia kuandaa mpango wa utekelezaji wa mwongozo wa hiari wa kuhakikisha Uvuvi mdogo unakuwa endelevu Tanzania kwani itasaidia wavuvi kutoka kwenye dimbwi la umaskini na kujiongezea kipato kutokana na uvuvi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527