WAZIRI WA AFYA ATOA TAMKO GHARAMA KUBWA ZA HOTELI KWA WANAOWEKWA KARANTINI KWA UGONJWA WA CORONA


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amewaagiza wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa yote nchini kuainisha hoteli ama sehemu zenye gharama nafuu, ambazo wasafiri wanaoingia nchini watakaa kwa siku 14 ili kuona kama wameambukizwa virusi vya corona au la.

Waziri Ummy Mwalimu ametoa agizo hilo kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter, baada ya kusambaa kwa picha ya video inayomuonesha msafiri mmoja akilalamikia kitendo cha kuwekwa kwenye hoteli zinazotoza gharama kubwa.

“Tumepokea hii changamoto ya sehemu zilizobainishwa kwa ajili ya 14-days mandatory isolation kwa wasafiri waliotoka nchi zilizoathirika zaidi na #COVID19, nawaelekeza maRC/RAS wa Mikoa yote kubainisha Hoteli/Sehemu ambazo wasafiri wengi watamudu gharama,” amesema Waziri Ummy Mwalimu.

Machi 22 mwaka huu, wakati akilihutubia Taifa kueleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na serikali ili kukabiliana na virusi vya corona, Rais John Magufuli alitangaza wasafiri wote watakaoingia nchini kutoka mataifa yaliyoathirika zaidi na virusi vya corona watalazimika kufikia sehemu za kujitenga na kukaa huko kwa muda wa siku 14 kwa gharama zao.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527