Picha : DC MBONEKO AKAGUA MIRADI YA MAJI WILAYA YA SHINYANGA...AHIMIZA WANANCHI KUTUNZA MIUNDOMBINU YA MAJI



Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji vya Mwang’osha, Lyabusalu pamoja na Mwiseme, na kuwataka wananchi waitunze miundombinu ya maji na kutoiharibu.

Mboneko amefanya ziara hiyo leo Machi 25,2020, ambapo alikuwa akikagua utekelezaji wa miradi hiyo ya maji hatua ilipofikia, ili ianze kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi.

Alisema Serikali ya awamu ya tano inatumia fedha nyingi sana ili kutekeleza miradi hiyo ya maji kwa wananchi, hivyo atasikitika endapo atasikia baadhi ya watu wameharibu miundombinu hiyo ya maji, na kuwataka wananchi kila mmoja awe mlinzi wa mwenzake ili kuitunza miundombinu ya miradi hiyo.

“Nawapongeza kwanza wananchi kwa kujitoa kuchangia shughuli hizi za maendeleo za utekelezaji wa miradi ya maji kwa kuchimba mitaro, pamoja na kutandaza mabomba ya maji, huu ndiyo uzalendo ambao Serikali tunautaka, na sisi tutahakikisha changamoto zote ambazo zinawakabili wananchi zinatatuliwa,” alisema Mboneko.

“Pia nawaomba muitunze miundombinu hii ya miradi ya maji na kutoiharibu, na wale ambao wanataka kuihujumu toeni taarifa mapema ili tuwachukulie hatua, na ambao watatafuna fedha za uendeshaji wa miradi hii ya maji watazitapika,” aliongeza.

Katika hatua nyingine aliwataka wananchi kuchukua tahadhari ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona, kwa kunawa mikono kwa sababuni kwa maji ya kutiririka , pamoja na kutoshikana, hali ambayo itawasaidia kuepukana na maambukizi hayo.

Naye Kaimu Meneja Wakala wa Maji vijijini wilaya ya Shinyanga (Ruwasa), Emmanuel Nkopi, alisema miradi hiyo ya maji kwenye vijiji hivyo vitatu, utekelezaji wake ulianza Februari mwaka huu na unatarajiwa kukamilika Aprili 15 mwaka huu, ambapo baadhi ya miradi tayari imeshaanza kutoa huduma ya maji kwa wananchi.


TAZAMA PICHA HAPA CHINI

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko (katikati) mwenye kilemba Chekundu) akiwa kwenye ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji katika wilaya ya Shinyanga leo Jumatano Machi 25,2020. Picha zote na Marco Maduhu - Malunde 1 blog

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko (katikati mwenye kilemba chekundu) akiendelea na ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwataka wananchi wa wilaya ya Shinyanga waitunze miundombinu ya maji.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwataka wananchi wa kijiji cha Mwang'osha wawe wazalendo katika nchi yao kwa kujitoa kuchangia shughuli za maendeleo na siyo kuwa sehemu ya kukwamisha miradi hiyo na kuzuia mabomba yasipite kwenye majaruba ya mpunga.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akizungumza na wananchi katika kijiji cha Mwiseme Kata ya Solwa na kuwapogeza kwa kujitoa kuchangia shughuli za maendeleo ikiwamo ukarabati wa Zahanati ya kijiji hicho.

Kaimu Meneja Wakala wa Maji Vijijini wilaya ya Shinyanga (Ruwasa), Mhandisi Emmanuel Nkopi, akitoa maelezo kwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga namna miradi ya maji inavyotekelezwa kwenye vijiji hivyo vitatu.

Diwani wa Kata ya Solwa Awadhi Abood, (wa pili kushoto) akipongeza utekelezaji wa miradi ya maji safi na salama kwa wananchi.

Mwananchi Richard Buswege mkazi wa kijiji cha Mwiseme Kata ya Solwa wilaya ya Shinyanga akiipongeza Serikali kwa utekelezaji wa miradi hiyo ya maji kwa wananchi.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko (katikati)akikagua uchimbaji wa mitaro ya mabomba katika mradi wa maji kijiji cha Mwang'osha.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akitoa maelekezo kwa msimamizi wa kituo cha kuchotea maji katika cha majengo kijiji cha Lyabusalu wilaya ya Shinyanga jinsi ya kutoa huduma ya maji kwa wananchi pamoja na umakini wa kutunza fedha anazo uza maji.

Wananchi wakiendelea na huduma ya uchotaji wa maji safi na salama katika kitongoji cha Majengo kijiji cha Lyabusalu wilaya ya Shinyanga.

Baadhi ya wananchi katika kijiji cha Mwang'osha wakiwa na Majembe kuendelea na zoezi la uchimbaji wa mitaro ya mabomba ya maji.

Baadhi ya wananchi katika kijiji cha Mwang'osha wakiwa na majembe kuendelea na zoezi la uchimbaji mitaro ya mabomba ya maji.

Diwani wa Kata ya Solwa Awadhi Abood (kushoto) akitoa maelezo kwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko namna wananchi wa kijiji cha Mwiseme walivyo jitoa kukarabati ujenzi wa Zahanati ya kijiji hicho.

Ukarabati wa Zahanati ya  kijiji cha Mwiseme ukiendelea.

Baadhi ya wananchi wa Solwa, ambao wamegoma kutoka kwenye njia ya mradi wa maji Ziwa Victoria ambayo itaoka Ihelele kwenda Shinyanga mjini, ambapo walishalipwa fidia lakini wamegoma kutoka  kwenye maeneo hayo, wakiagizwa na mkuu wa wilaya waondoke haraka sana, na wale ambao kuna utata Kashwasa akaiagiza ikapime upya maeneo hayo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akinawa mikono kwa maji tiririka na sabuni pamoja na wajumbe aliokuwa ameambatana nao kujikinga na maambukizi ya virusi ya Corona kwenye ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji katika wilaya ya Shinyanga

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akinawa mikono kwa maji tiririka na sabuni pamoja na wajumbe aliokuwa ameambatana nao kujikinga na maambukizi ya virusi ya Corona kwenye ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji katika wilaya ya Shinyanga.

Na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527