MAKONDA ATOA MAAGIZO KATIKA KUKABILIANA NA VIRUSI VYA CORONA...."KUWE NA NDOO ZA KUNAWIA, MISONGAMANO MARUFUKU"


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amepiga marufuku msongamano wa abiria katika vyombo vya usafiri, maeneo ya ibada, benki na mengineyo jijini humo ili kujikinga na ugonjwa wa virusi vya corona.

Aidha, ametoa maelekezo katika kujikinga na virusi hivyo kuwa ziwekwe ndoo za kunawia mikono zenye maji yanayotiririka na dawa za kusafishia mikono katika maeneo yote ya hoteli na nyumba za kulala wageni, kumbi za starehe na kwenye mashine za kutolea fedha (ATM).

Maeneo mengine ni kwenye baa, maduka, maeneo ya ibada, maeneo ya taasisi za serikali na zisizo za serikali, shule, vituo vya afya, bandari, viwanja vya ndege na katika kila kaya.

“Wamiliki wote wa mabasi makubwa na madogo ya kubeba abiria yanayoingia na kutoka na yaliyopo ndani ya Mkoa wa Dar es Salaam, boti za mwendo kasi, treni/Shirika la Reli Tanzania (Tazara), Uongozi wa Stendi kuu ya Mabasi Ubungo na mengineyo waweke sehemu za kunawa mikono kwa maji yanayotiririka na kwa sabuni na utekelezaji wa suala hili ukamilike ndani ya siku tatu kuanzia leo Machi 16.

Ameongeza kuwa ugonjwa huo haupo Tanzania lakini kutokana na muingiliano mkubwa wa Mkoa wa Dar es Salaam, mikoa mingine na nchi nyingine ni muhimu kuchukua tahadhari ili kuzuia ugonjwa huo usiingie nchini.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527