WAZIRI JAFO AAGIZA ALIYEKANYAGA KITABU CHA DINI ASIMAMISHWE KAZI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, Selemani Jafo amemuagiza mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro kumsimamisha kazi Daniel Elimringi ambaye video zinazosambaa katika mitandao ya kijamii zinamuonyesha akikanyaga kitabu cha dini.






Jafo ametoa agizo hilo leo Ijumaa Februari 7, 2020 mjini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu video hiyo iliyozua gumzo mitandaoni.

Amesema Elimringi ni ofisa biashara wa wilaya hiyo, “mtumishi huyo yupo chini ya ofisi ya Rais Tamisemi,  tukio lile ukiliangalia kwenye mitandao ya kijamii halileti afya njema kwa nchi yetu ambayo ina utulivu na amani lakini wananchi wake wanaheshimiana kwa misingi ya imani mbalimbali”

“Mimi ni waziri ninayesimamia tawala za mikoa na Serikali za mitaa ambayo Halmashauri ya Kilosa ni miongoni mwa halmashauri ninazozisimamia maana yake na mtumishi huyo ni miongoni mwa watumishi walio chini ya Tamisemi. Nimemuagiza mkurugenzi kumsimamisha kazi.”

Ameongeza, “nimemuagiza mkurugenzi amsimamishe kazi na afanye uchunguzi na kamati ama mamlaka yake ya nidhamu iweze kuchukua hatua kwa kadri itakavyoona inafaa mara baada ya uchunguzi huo.”

Amesema kitendo hicho hakileti picha nzuri kwa Watanzania wanaoheshimiana.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527