MIILI YA ASKARI WALIOFARIKI KWA AJALI NJOMBE YAAGWA NA MAMIA YA WANANCHI


Na Amiri Kilagalila-Njombe
Mamia ya wananchi wamejitokeza hii leo katika viwanja vya jeshi la polisi mkoani Njombe kuaga miili ya askari watatu waliofariki katika ajali mapema alfajiri ya tarehe tatu ambapo ajali hiyo imehusisha basi la abiria kampuni ya sharon lenye namba za usajiri T349 CXD na gari la polisi lenye namba za usajili pt 3734.



Askari waliofariki katika ajali hiyo ni namba H 4401 Marianus Said Hamissi,namba H6802 pc Michael Mwandu na askari namba H 7486 pc Hery Athmani ambapo wote wamesafirishwa kuelekea makwao kwaajili ya mazishi

Akizungumza wakati wa kuaga miili ya askari hao mkuu wa mkoa wa Njombe Cristopher Ole Sendeka amesema, serikali imepoteza vijana mhimu ambao wamefariki wakati wakienda kulitumikia taifa na kuwataka askari wengi kuwa wavumilivu katika kipindi hiki kigumu.

“Ajali hii imeondoa vijana wetu watatu,wawili wapo Moi tumewakimbiza jana kwa ndege na wengine wapo kwenye hospitali yetu ya kibena na hakika vyombo vyote vitasimamia kujua ukweli wa tukio hili na aliyefanya dhambi hii kwa uzembe atachukuliwa hatua za kisheria”alisema Ole Sendeka

Hamis  Issa ni kamanda wa polisi mkoa wa Njombe amewashukuru wakazi wa mkoa wa Njombe kwa kujitokeza kwa wingi pamoja na kujitolea michango yao kuhakikisha askari wote waliofariki wanasafirishwa kuelekea kwao kwaajiri ya mazishi.

“Wananchi mmeonyesha ni jinsi gani mna upendo na vijana wenu,na hawa waliofariki kwa kweli wamefariki wakiwa wanaenda kutimiza jukumu la kisheria,tunawashukuru sana”alisema Hamis Issa

Solanus Mhagama ni mmoja wa wakazi mkoani hapa ameonyesha kusikitishwa na kifo cha askari hao ambao walikuwa bado vijana wadogo na hivyo kuiomba serikali kuweka matuta pamoja na kutanua barabara hiyo ili kuepusha ajali katika eneo hilo ambalo lina mlima mkali.

Ajali hiyo iliyosababaishwa na mwendokasi wa gari ya abiria ilipelekea  vifo  vitatu vya askari wa polisi kikosi cha kutuliza gasia mkoani Njombe huku wengine tisa wakiendelea na matibabu katika hospitali ya mji Njombe Kibena na hospitali ya taifa Mhimbili.

Ibada ya kuagwa miili hiyo imehudhuliwa na viongozi wa dini mbalimbali ambapo wametumia fulsa hiyo kuwa taka wananchi kufuata sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali zinazosababishwa  na uzembe.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post