Waziri Mhagama Aridhishwa Na Hatua Za Ujenzi Wa Jengo La NEC Dodoma

NA.MWANDISHI WETU
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama ametembelea na kukagua hatua ya ujenzi wa jengo la Ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi zilizopo eneo la Njedenwa Jijini Dodoma na kusema ameridhishwa na hatua iliyofikiwa.

Alikagua mradi huo, Januari 07, 2020 ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Mhe. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aliyoyatoa Novemba 18, 2019 alipotembelea na kukagua mradi huo na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi na kutoa maagizo hayo baada ya TBA kusimamisha zoezi la ujenzi kwa ongezeko la gharama za  kutoka bilioni 13 hadi bilioni  32 na hivyo kumtaka Waziri Mhagama kufuatilia.

Ziara ya Waziri Mhagama imebaini maendeleo mazuri ya ujenzi na kufikia hatua ya asilimia 75 baada ya Tume hiyo kuingia mkataba SUMA JKT kuwapongeza wakandarasi kwa hatua hiyo wanayoendelea nayo.

“Kwa kipindi chote ambacho SUMA JKT imeendeela na kazi ya ujenzi wa jengo hili hali inaridhisha na ni vyema kuhakikisha mnaendana na kasi inayotakiwa kwa kuzingatia gharama zilizokubalika za bilioni 16,”Alisistiza Waziri Mhagama

Alieleza kuwa ujenzi wa majengo ya Serikali ni moja ya hatua za kuhakikisha zoezi la kuhamisha watumishi Dodoma linafanikiwa kwa kuendelea kuweka miundombinu rafiki ya ofisi zao.

“Mpaka sasa tayari watumishi wapatao 14868 wameshahamia hapa Dodoma hivyo tutaendelea kuandaa mazingira ikiwemo ujenzi wa ofisi hizo kwa kuzingatia kazi ya Uratibu huo ipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu,”alisema Mhagama

Alifafanua kuwa, kukamilika kwa jengo hilo kutasaidia kuhakikisha watumishi wa ofisi hiyo wanatoa huduma vizuri kwa kuzingatia mwaka 2020 ni mwaka wa uchaguzi mkuu ambapo itasadia utendaji wa kazi.

Waziri Mhagama ameendelea kueleza kuwa   , miongoni mwa majukumu ya Ofisi yake ni kuhakikisha inaratibu shughuli zote za kuhamisha watumishi wa Serikali na kuweka mazingira mazuri ya ofisi zao ili kuendelea kuitumikia nchi kwa weledi na kujiletea maendeleo yao kwa kutoa wa huduma bora zinazostahili.

Kwa upande wake mmoja wa wasimamizi wa ujenzi wa majengo hayo Mhandisi Michael Mussa alieleza kuwa, wataendelea kufanya kazi kwa viwango vinavyotakiwa ili kuwa na majengo yenye ubora kwa kuzingatia gharama zilizofikiwa kwenye mkataba wa ujenzi huo.

“Tumefarijika kwa ujio wa Mhe. Waziri na tunaahidi tutajenga kwa kipindi kilichopangwa kwa kuzingatia gharama zilizopo kwenye mkataba wa ujenzi huu,”alieleza Mhandisi Michael.

=MWISHO=


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments