WAZIRI MWAKYEMBE : UKOMO WA WAANDISHI WA HABARI WASIOKUA NA ELIMU KUANZIA DIPLOMA NI DESEMBA 2021


Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo,Dkt.Harrison Mwakyembe akizungumza na Viongozi wa Mkoa wa Singida pamoja na wadau wa tasnia ya habari Januari 22,2020 alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kukagua mitambo ya usikivu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) iliyoko Mikumbi lengo ikiwa ni kuimarisha usikivu wa shirika hilo ambao kwa sasa umefikia asilimia zaidi ya 70 nchini.


Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Dkt. Ayoub Ryoba akizungumza Januari 22,2020 wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Dkt.Harrison Mwakyembe yenye lengo la kukagua mitambo ya usikivu ya shirika hilo iliyoko Mikumbi mkoani Singida lengo ikiwa ni kuimarisha usikivu wa shirika hilo ambapo amesema kwa sasa usikivu umefikia asilimia zaidi ya 70 nchini.
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari - MAELEZO, Rodney Thadeus akiwasisitiza wanahabari wa mkoa wa Singida (hawapo pichani) umuhimu wa kuwa na kitambulisho cha Mwanahabari ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa uhuru na kwa mujibu wa sheria katika ziara ya kikazi ya Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison Mwakyembe Mkoani hapo yenye lengo la kukagua mitambo ya usikivu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) iliyoko Mikumbi lengo ikiwa ni kuimarisha usikivu wa shirika hilo ambao kwa sasa umefikia asilimia zaidi ya 70 nchini pamoja na kukutana na wadau wa tasnia ya habari mkoani hapo iliyofanyika Januari 22,2020.
Waziri wa Habari,Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison Mwakyembe pamoja na Naibu wake, Juliana Shonza wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Rehema Nchimbi pamoja na viongozi wengine mara baada ya kikao kilichofanyika Januari 22,2020 katika ofisi za mkoa huo kilichokua na lengo la kuzungumzia ziara ya viongozi hao mkoani hapo.
Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison Mwakyembe akiongozwa na Eng.Upendo Mbele pamoja na Mkama kukagua mitambo ya usikivu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) iliyoko Mikumbi Mkoa wa Singida wakati wa ziara yake ya kukagua mitambo ya Shirika hilo lengo ikiwa ni kuimarisha usikivu ambao kwa sasa umefikia asilimia zaidi ya 70 nchini iliyofanyika Januari 22,2020.
Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe pamoja na Naibu wake Juliana Shonza wakisaini kitabu katika Ofisi ya Mkoa wa Singida walipofika katika ziara ya kikazi mkoani hapo Januari 22,2020.

Na Shamimu Nyaki –WHUSM, Singida.
WAZIRI wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison Mwakyembe amesisitiza kuwa itakapofika Desemba mwaka 2021 ndio mwisho wa waandishi wa habari wasiokua na elimu kuanzia ngazi ya stashahada kufanya kazi hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma ya habari ya Mwaka 2016.

Waziri Mwakyembe ametoa kauli hiyo jana Mkoani Singida alipokuwa anazungumza na wadau wa tasnia ya habari ambapo amewataka waandishi hao kutambua kuwa kuanzia mwaka 2022 wale ambao hawatakua na vigezo kulingana na Sheria ya Huduma za Habari hawatakua na nafasi wala sifa ya kuitwa Waandishi wa Habari.

“Uandishi wa habari ni taaluma kama taaluma nyingine na sio kimbilio la wale ambao wamefeli katika masomo au waliokosa kazi ya kufanya,hivyo naomba mtambue kuwa mwaka 2021 ndio mwisho wa waandishi wasiokua na elimu ya uandishi wa habari kuanzia ngazi ya stashahada”amesema Mwakyembe.

Aidha Dkt.Mwakyembe amesema kuwa Ibara ya 18 d ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaeleza kuwa kila mwananchi ana haki ya kupata taarifa sahihi hivyo ni jukumu la wanahabari kuhakikisha kuwa wanatoa taarifa ambazo ni sahihi kutoka kwa watu sahihi na kuzifikisha kwa walengwa kwa usahihi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhandisi Paskasi Mlagiri ameongeza kuwa mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi hivyo wanahabari wasitumike kuchafua watu,kuandika habari za uongo pamoja na kuepuka kupewa rushwa na watu wanaotaka watumie kalamu zao kuwatafutia kura na badala yake waandike habari za ukweli ambazo zitalinda amani na usalama wa nchi yetu.

“Tumeni kalamu zenu vizuri ili msije kuhatarisha amani ya nchi yetu na pia jiepusheni na kuandika habari kwa kutegemea kupewa pesa na wale wanaowapa habari ili msije mkaingia katika mikono ya Sheria” alisema Eng.Mlagiri.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari Maelezo, Rodney Thadeus amewataka waandishi wa habari kuhakikisha kuwa wanakuwa na kitambulisho cha mwanahabari popote wanapokuwa wanatimiza majukumu yao kwani ndio utambulisho wa tasnia hiyo huku akieleza kuwa vitambulisho vya wanahabri hao kwa mwaka huu tayari vinapatikana katika ofisi yake.

Awali,Waziri Mwakyembe alifanya ziara ya kukagua mitambo ya usikivu wa redio ya Shirika la Utangazaji TBC iliyopo katika eneo la Mikumbi mkoani hapo ambapo ameeleza kuwa Serikali inaendelea na juhudi za kuimarisha usikivu wa redio ya Shirika hilo nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo Dkt.Ayoub Ryoba amesema kuwa mitambo miwili ya Khts 2 kwa kila mmoja imeshawasili nchini tayari kwa kufungwa ili kuongeza usikivu katika maeneo mengi nchini ambapo kwa sasa usikivu umefikia asilimia zaidi ya 70.

“Usikivu wa Shirika la Utangazaji TBC kwa mwaka 2016 ulikua asilimia 54, mwaka 2019 asilimia 67 na mwaka huu tunategemea kufikia asilimia zaidi ya 70 lengo ni kufikia watu wengi zaidi”. Alisema Dkt.Ryoba.

Hata hivyo katika ziara hiyo Waziri Mwakyembe amepata nafasi ya kupata historia fupi ya wanawake wawili ambao ni Litti Hema pamoja na litti Kidanka waliopigania uhuru wa kabila la wanyaturu uliofanywa na Mwalimu Alfred Ringi ambapo imeleeza ushiriki wa kila mmoja katika kukomboa kabila hilo kwa kutumia mvua na nyuki ambapo Waziri amemuagiza mwalimu huyo kuendelea kutafuta undani wa historia hiyo ili
Serikali iweze kuihifadhi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527