SERIKALI YAJIPANGA KUTUMIA FILAMU KUTANGAZA VIVUTIO VYA UTALII KIMATAIFA

Na Anitha Jonas – WHUSM,Dar es Salaam.

Viongozi wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo na Wizara ya Maliasili na Utalii wapanga mkakati wa kutumia sekta ya filamu kuwavutia watengenezaji wa fila
mu kutoka nje kutumia vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania.

Kikao cha kupanga mkakati huo kimefanyika leo jijini  Dar es Salaam baina ya wizara hizo ambapo walijadili namna ya kuboresha mazingira ya katika utoaji wa huduma za waandaji wa filamu kutoka nje ya nchi na kuwavutia kuja kwa wingi kutumia vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini kufanya kazi zao.

Akizungumza katika kikao hicho Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo alisema katika kudumisha mahusiano ya wizara hizo mbili ambazo zinamwingiliano kutokana na majukumu yake wizara  itaangalia maslahi mapana ya usalama wa taifa katika kuboresha mazingira ya uandaaji wa filamu za wadau kutoka nje ya nchi.

“Tumeunda timu kutoka pande zote mbili ambayo itaenda kuangalia  namna ya kuboresha mazingira yatakayowavutia waandaji  wa filamu na makala kutoka nje ya nchi kuja kwa wingi zaidi kufanya kazi zao katika vivutio vyetu, na watakapomaliza  kazi hiyo wataleta ushauri wao, lengo ni kuhakikisha nchi inafanikiwa kukuza uchumi,’’ alisema Dkt.Possi.


Pamoja na hayo Dkt.Possi alisema  kuwa katika kikao hicho walijadili  kuweka msisitizo pia kuhusu kuhakikisha utoaji wa vibali kwa waandaji wa flamu za nje unakuwa wa haraka na suala hilo limezingatiwa kwa maslahi ya Taifa .

Kwa upande wa Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Prof.Adolf Mkenda alisema nchi inavivutio vingi vizuri na baadhi ni vipya hivyo kwa kutumia sekta ya filamu inaweza kutangaza vivutio hivyo kwa wingi pasipo gharama kwani gharama ya kutangaza  vivutio ni kubwa.

“Tunaangalia namna yakukuza utalii kupitia filamu sababu ni moja ya njia rahisi ya kutangaza vivutio vya utalii  ni filamu,mfano wa Filamu ya ‘Serengeti  Shall Never Die’ ilifanya vizuri katika kutangaza mbuga ya Serengeti  pia ilisaidia  kuongeza idadi ya  watalii katika mbuga hiyo, hivyo tumeona tuangalie namna ya kuboresha mazingira ya kuwavutia waandaaji hao wa filamu kuja kufanya kazi zao katika vivutio vyetu kama Katavi,Gombe,Burigi,Rubondo na vinginevyo,’’alisema Prof.Mkenda.

Aidha, Katibu Mkuu huyo wa  Wizara ya Maliasili na Utalii aliendelea kusema kwa sasa vivutio vinavyofanya vizuri katika utalii ni Serengeti, Ngorongoro ,Kilimanjaro,Manyara , Tarangire na Mikumi  na Tanzania inavivutio vingi sana hivyo tukitumia fursa ya waandaji wa filamu wa nje ya nchi itasaidia kuongeza utalii wa vivutio ambavyo bado havijapata umaarufu.

Halikadhalika nae Kaimu Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Sanaa kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bibi.Joyce Fisoo alitoa ombi kwa Wizara ya Maliasili na Utalii  kusaidia kutoa ufadhili wa masomo kwa wataalamu wa uandaaji wa kazi za filamu nchini kwani kwa sasa kuna  upungufu  wataalam hao na hii ni changamoto kwa waandaji  wa filamu hizo wanapokuja nchini na kuhitaji wataalamu hao kutoka nchini.

“Katika  kuboresha  sekta ya uandaaji wa filamu za kisasa na zenye ubora  ningeiomba    Wizara ya  Maliasili na Utalii kutoa ufadhiili wa masomo  ya uandaaji wa kazi za filamu kwa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC)  kwani kutasaidia kuboresha  vipindi vya kutangaza  vivutio vilivyopo nchini kupitia Safari Chaneli  ambayo ni chaneli ya kutangaza utalii”alisema Bibi.Fisoo.

Hatahivyo nae Kaimu Kaimu Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Tanzania Dkt.Kiagho Kilonzo alisema ofisi yake imeandaa kikao na wadau wanaleta watengenezaji wa filamu kutoka nje ya nchi  kwa lengo la kuzungumza nao na kufahamu  ni changamoto gani wanazoziona katika kuwavutia watengenezaji hao wa filamu kuja kufanya kazi nchini nini kifanyike ili kuboresha na kufikia malengo ya kutangaza utalii wa vivutio vilivyopo nchini.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527