ROSE MUHANDO AFUNGUKA YALE YALIYOJIRI WAKATI AKITOLEWA MAPEPO KANISANI

Mwimbaji wa nyimbo za Injili Rose Muhando hatimaye amezungumza kuhusu video iliyosambaa sana mitandaoni mnamo 2018.


Huku watu wakiendelea kuwa na maswali kuhusu kudidimia kwake, video ya msanii huyo akijibingirisha sakafuni akiwa amelala chali iliwaacha wengi na hisia kinzani.

Akizungumza na SDE ya Kenya, Rose alikiri kwamba anafahamu fika kuwa tukio hilo lilitokea katika kanisa la Pasta Ng’ang’a.

Hata hivyo, hana ufahamu wowote wa namna alijipata katika kanisa hilo ama kile kilichojiri wakati alikuwa anaondolewa mapepo.

Mwimbaji huyo anayesifika sana kwa wimbo Yesu Nibebe, pia alikanusha madai ya kumuomba mchungaji huyo mwenye utata kumuombea uponyaji kama ilivyobainika awali.

Muhando anaamini kuwa alifungwa macho kuingia katika kanisa hilo kwani alipoteza fahamu kipindi kizima cha maombi.

Rose pia alitambua kwamba Ng’ang’a alimpigia simu baada ya kufahamu alikuwa mgonjwa na akajitolea kumuombea.

Msanii huyo ambaye alikumbana na maumivu makali tumboni alikubali ombi la pasta huyo na kutembelea kanisa lake.

“Pasta Ng’ang’a alinialika katika kanisa lake na niliwasili mapema siku moja. Wakati wa kukombolewa, nilikuwa na maumivu makali tumboni na aliniambia ataniombea. Nilizirai baada ya kusikia maneno yake matatu na hadi leo, siwezi nikaelezea kile kilitokea," alisema Rose.

Muhando, kisha alikiri kwamba wanawe wana baba tofauti na wanaendelea vyema popote walipo na pia wanaume walikuwa wamezoea kumwacha baada ya kujifungua.

“Watoto wangu wote wako shuleni. Wote wana baba tofauti kwa sababu wote waliniacha wakati nilikuwa na mimba ama wakati mtoto alikuwa mchanga," alifunguka Rose.

Credit: Tuko Kenya


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527