MO DEWJI AKUTANA NA RAIS WA FIFA NA KUFANYA NAYE MAZUNGUMZO


Wakati Simba ikitarajiwa kushuka dimba la Taifa leo saa moja usiku kuikaribisha Namungo FC kwenye mechi ya Ligi Kuu Bara, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya klabu hiyo, Mohamed 'Mo' Dewji, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Shirikisho la Soka Duniani (Fifa), Gianni Infantino.


Katika mazungumzo yao, wawili hao waligusia mipango ya Fifa kuendeleza soka barani Afrika, Dewji akieleza matumaini yake juu ya maendeleo ya mpira wa miguu barani katika uongozi wa Infantino.

"Kwa kweli, nimefurahishwa sana kwa dira na shauku ya kuendeleza mpira wa ushindani na shauku Afrika. Nia ya Fifa ni kuboresha maendeleo ya mpira.

"Najua chini ya uongozi wa Gianni, mpira wa miguu kwenye bara letu, utapiga hatua zaidi," Dewji alieleza baada ya mazungumzo yake na bosi huyo wa Fifa.

Aidha, Dewji alimkabidhi Infantino jezi ya Simba ikiwa imeandikwa jina la rais huyo ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kupiga vita rushwa michezoni na ufujaji wa fedha uliokuwa ukifanywa ndani na nje ya shirikisho hilo kwa wanachama wake.

Dewji, mmoja wa mabilionea vijana barani Afrika, ameifanya Simba kuwa miongoni mwa klabu zinazoendeshwa kwa kisasa Afrika na sasa inatajwa kama timu inayotarajiwa kuwa tishio ndani ya miaka michache ijayo barani Afrika.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527