MAREKANI YATANGAZA VIKWAZO VIPYA DHIDI YA IRAN


Utawala wa rais Donald Trump wa Marekani umetangaza awamu mpya ya vikwazo vya kiuchumi kwa Iran kufuatia mashambulizi ya makombora yaliyofanywa na Tehran kwenye kambi za jeshi la Marekani nchini Iraq. 

Siku ya Ijumaa, Wizara ya Fedha ya Marekani ilitangaza kuwawekea vikwazo maafisa 8 wa ngazi za juu wa Iran akiwemo Mohsen Rezai, Katibu wa Baraza la Kuainisha Maslahi ya Mfumo wa Kiislamu, Ali Shamkhani, Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran na Mohammad Reza Naqdi Mratibu katika Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC). 

Kwa mujibu wa vikwazo hivyo wakuu hao wa Iran hawataweza kuingia Marekani na iwapo wana mali zozote Marekani basi zitazuiwa. 


Aidha taarifa ya Wizara ya Fedha ya Marekani mbali na kuwawekea vikwazo maafisa hao wa Iran pia imetangaza vikwazo dhidi ya mashirika 18 ya Iran ambayo yanashughulika katika sekta za chuma na madini na hali kadhalika mashirika matatu yaliyoko nchini China ambayo yanahusika katika kununua chuma kutoka Iran.

Taarifa ya Wizara ya Ulinzi ya Marekani imesema: "Sambamba na kutangazwa vikwazo hivyo, Trump ametia saini amri ambayo itaweka vizingiti katika vyanzo vya fedha zinazotumiwa na Iran katika sekta za ujenzi wa miundo msingi, madini na ufumaji.

Mapema wiki hii Iran ilifanya mashambulizi kwenye kambi nchini Iraq ili kulipa kisasi baada ya Marekani kumuua kamanda wa ngazi ya juu wa jeshi lake, Qassem Soleimani.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527