WASAIDIZI WA KISHERIA 80 WAPIGWA MSASA SHINYANGA...HAKIMU ATAKA WAEPUKE RUSHWA KUSAIDIA WANYONGE


Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Kahama Evodia Kyaruzi akizungumza na wahitimu wa mafunzo ya awali ya Sheria (Wasaidizi wa kisheria) hawapo pichani.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo wakimsikiliza kwa makini Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Kahama Evodia Kyaruzi.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo wakimsikiliza kwa makini Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Kahama Evodia Kyaruzi.

 Mkurugenzi wa shirika la PACESHI, Perpetua Magoke akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali ya sheria kwa wasaidizi wa kisheria kutoka Halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga

Meneja mradi wa kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa wote mjini na Vijijini kutoka shirika la PACESHI, John Shija akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali ya sheria kwa wasaidizi wa kisheria kutoka Halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo ya awali ya sheria wakiwa katika picha ya pamoja na Mgeni rasmi Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Kahama Evodia Kyaruzi.
Viongozi wakuu wa Shirika la PACESHI wakiongozwa na mkurugenzi wa Shirika hilo Bi,Perpetua Magoke wakiwa katika picha ya pamoja na Mgeni Rasmi hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Kahama Evodia Kyaruzi .


Na Salvatory Ntandu - Malunde 1 blog 

Wahitimu 80 wa mafunzo ya awali ya sheria kutoka Halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga, wametakiwa kutojihusisha na vitendo vya rushwa wanapotoa huduma kwa wananchi katika maeneo wanayoishi ili kutokomeza vitendo vya jinai katika jamii.

Kauli hiyo imetolewa Desemba 16,2019  na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Kahama, Evodia Kyaruzi wakati akifunga mafunzo ya siku 15 ya wasaidizi wa kisheria yaliyotolewa na shirika lisilo la kiserikali la Paralegal Aid Center Shinyanga (PACESHI) yaliyofanyika mjini Kahama.

“Toeni huduma za kisheria kwa wazee wasiojiweza,watoto na akina mama wajane ambao haki zao zinaonekana kupokwa na watu wengine ili waweze kupata masaada zaidi kutoka vyombo vya sheria kama vile Mahakama”,alisema Kyaruzi.

Alisema kwenye jamii kuna matukio mengi yanajitokeza kama vile ubakaji kwa watoto,vipigo vya akina mama,migogoro ya Mirathi,na ndoa za watoto za watoto chini ya miaka 18 hivyo ni budi kuhakikisha wanaisadia jamii kuondokana na jinai hizi kutokana mafunzo ya sheria mbalimbali walizofundishwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la PACESHI, Perpetua Magoke alisema endapo wasaidizi hao wa kisheria wakifanya kazi kwa weledi katika jamii wanazotoka itasaidia kupunguza matukio ya jinai ambayo yanajitokeza mara kwa mara katika mkoa wa Shinyanga.

“Mmefundishwa sheria mbalimbali hakikisheni elimu mlioipata inaleta matokeo chanya na tija katika jamii zenu kwa kuyasaidia makundi ya watu waliosahaulika katika jamii kama vile wazee na walemavu” ,alisema Magoke.

Kwa upande wake Meneja mradi wa kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa wote mjini na Vijijini kutoka shirika la PACESHI, John Shija alisema ili kukidhi mahitaji ya jamii kupata msaada wa kisheria PACESHI imeamua kutoa mafunzo hayo kwa wasaidizi wa kisheria 80 kutoka halmashauri za Msalala,Kishapu,Kahama mji,Manispaa ya Shinyanga,Ushetu na Halmashauri ya Shinyanga.

“Tumewafundisha sheria mama ya msaada wa kisheria (Legal Aid Act No 1/2017)ili watambue mbinu mbalimbali za kuwasidia wahitaji ili kupata msaada stahiki wa kisheria”,alisema Shija.

Esta Enock kutoka halmashauri ya msalala na Sita Said Mahonja kutoka Manispaa ya Shinyanga walisema mafunzo hayo yamekuwa msaada mkubwa kwao kwani awali walikuwa hawana uelewa kuhusiana na sheria ambapo kwa sasa wataweza kuwahudumia wananchi wengi kwa haraka sana.

Mafunzo hayo ya siku 15 yalianza mjini Kahama Disemba 2 mwaka huu na kuhitimishwa Disemba 16,2019.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527