MHITIMU WA DARASA LA SABA ADAIWA KUMPA UJAUZITO BINTI WA KIDATO CHA PILI...DC ASEMA MIMBA ZIMEGEUZWA ATM

Mwanafunzi wa kidato cha pili Sekondari ya Bunambiyu wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga nchini Tanzania mwenye miaka 17 amekatisha ndoto zake za kuendelea na elimu ya kidato cha tatu baada ya kudaiwa kupewa ujauzito na mwanafunzi aliyemaliza darasa la saba 2019.

Mwanafunzi huyo ambaye anatuhumiwa kumpa ujauzito mwanafunzi mwenzake alikuwa anasoma katika shule ya msingi Mwasubi kata ya Bunambiyu mkoani humo ambaye amechaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2020 katika sekondari ya Bunambiyu.

Akizungumza jana Ijumaa Desemba 27, 2019, baba mzazi wa mwanafunzi aliyepewa ujauzito, Elisha Mashilimu alisema mwanaye alibainika kuwa na ujauzito wa miezi mitatu baada ya kufanyiwa uchunguzi na kufukuzwa shule na kwa sasa yupo tu nyumbani.

Alisema binti yake alipohojiwa juu ya ujauzito huo alidai ni wa mwanafunzi ambaye amemaliza darasa la saba mwaka huu (jina tunalo) na kuripoti polisi ambapo mtuhumiwa alikamatwa huku kukiwa na utata kuwa ujauzito siyo wa mwanafunzi huyo bali ni kijana mwingine.

“Mwanangu anamtaja mwanafunzi huyo lakini baadhi ya watu wananieleza ujauzito huo siyo wa mwanafunzi aliyemtaja ni wa kijana mwingine ambaye tumeshindwa kumfahamu,” alisema Mashilimu.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mwasubi, Kongezya Kanagano shule aliyokuwa akisoma mwanafunzi, aliyedaiwa kumpa ujauzito mwanafunzi mwenzake alisema alimwita nakuzungumza naye lakini alidai ujauzito huo sio wa kwake anasingiziwa.

Mwalimu Kanagano alisema mwanafunzi aliyepewa ujauzito amekwisha muonya mara nyingi akiwa na vijana wengine. 

Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Talaba alisema ndoa na mimba za utotoni zimegeuzwa kuwa kama ATM kadi na baadhi ya watu kwa kuzitumia kujipatia fedha, huku akiwanyoshea kidole baadhi ya watendaji wa kata na walimu kuwalinda watuhumiwa.

Kwa mwaka 2018 zilitokea mimba 56 katika wilaya hiyo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527