DKT. JINGU : TAALUMA YA MAENDELEO NA USTAWI WA JAMII IWE CHACHU YA MABADILIKO KATIKA JAMII


Na Mwandishi Wetu Morogoro
Katibu Mkuu Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu amevitaka Vyuo na Taasisi za Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii nchini kutoa elimu itakayowasaidia wahitimu kuleta mabadiliko katika jamii zao na kuweza kujiajiri na kuajiri watu wengine kuliko kutegemea kuajiriwa.


Dkt.John Jingu ameyasema haya leo mkoani Morogoro wakati akifungua kikao kazi cha wakuu wa Vyuo na Taasisi za Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii nchini kilicholenga kubadilishana uzoefu kwa wakuu hao wa vyuo katika utendaji kazi na kujengeana uwezo ili Taasisi na Vyuo viweze kufanikisha malengo ya Taifa.

Dkt. Jingu amesema kuwa taaluma ya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii  lazima iwe nyenzo ya kutatua changamoto zilizopo katika jamii ikiwemo tatizo la ajira kwa vijana kwa kutoa taaluma itakayowapa fursa wahitimu kujiajiri kutokana na taaluma waliyopata.

“Umefika wakati sasa Taasisi na Vyuo kuja na Mpango Mkakati wa namna ya kutekeleza dhana ya kujiajiri  kwa lengo la kuzalisha wahitimu mahiri " alisema Dkt. Jingu.

Ameongeza kuwa Vyuo vya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii vimetoa mchango mkubwa sana katika kutatua changamoto za jamii na hivyo jamii kuthamini uwepo wa vyuo katika jamii na mafanikio yaliyoonekana  kwa vyuo hivyo yaonekane kwa kila chuo.

Aidha Dkt. Jingu amevitaka Vyuo hivyo kuanzisha Vituo vya kielektroniki vya ubunifu na maarifa (Digital Innovation Centre) ambao utarahisisha upatikanaji wa maarifa na ujuzi kwa haraka zaidi kuliko kusoma vitabu na itatoa fursa ya kupata maarifa katika muda mfupi.

“Natumaini ushiriki wetu katika kikao kazi hiki utatuongezea ari na ubunifu wa kazi katika maeneo yetu na mtazingatia mafunzo na maelekezo yatakayotolewa katika kuhakikisha vyuo vinatoa matokeo chanya kwa kuzalisha wataalam wenye ujuzi na maarifa ya kazi.   

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Jamii nchini Patrick Golwike amesema kuwa ili kujipambanua katika jamii umuhimu wa Kada ya Maendeleo ya Jamii inatakiwa kuwa na mbinu ya namna ambayo Vyuo vya Maendeleo ya Jamii itatoa wataalam wakaosaidia kuleta mabadiliko kwa jamii.

Naye Kamishna wa Ustawi wa Jamii nchini Dkt. Naftali Ng’ondi amesema kuwa Kada ya Ustawi wa Jamii ni moja kati ya Kada ambazo zina uwanda mpana wa kujiajiri na kuajiriwa hivyo Vyuo na Taasisi ya Ustawi wa Jamii zijikite katika kutoa elimu itakayowasaidia wahitimu hasa kujiajiri.

Wakuu wa Vyuo na Taasisi za Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii wamekutana mkoani Morogoro katika kikao kazi kilicholenga kutafuta namna bora ya taaluma ya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii katika kuleta mabadiliko katika jamii.

MWISHO.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527