OFISI YA SERIKALI YACHOMWA MOTO...DIWANI WA CHADEMA ASHIKILIWA

Na Daniel Mjema na Janet Joseph, mwananchi
 Nani wamehusika? hili ndilo swali linawaumiza vichwa wapelelezi baada ya watu wasiojulikana kuchoma moto ofisi ya Serikali ya mtendaji wa kata ya Soweto katika Manispaa ya Moshi.

Tukio hilo limetokea wakati mchakato wa uchaguzi wa serikali za mitaa ambao umekumbwa na utata ukiendelea, lakini baadhi ya watu wamelihusisha na uhalifu wa kawaida.

Taarifa kutoka eneo la tukio zinaeleza kuwa watu hao walichoma ofisi hiyo kwa kutumia mafuta ya petroli na kusababisha baadhi ya nyaraka na samani za ofisi kuungua.

Tayari watu kadhaa wanashikiliwa na polisi, akiwamo Collin Myuta ambaye ni diwani wa Kata ya Soweto (Chadema), huku chama hicho kikitaka weledi katika uchunguzi wa tukio hilo. Katibu wa Chadema mkoani Kilimanjaro, Basil Lema alisema haelewi sababu za polisi kumhusisha diwani wao na tukio hilo na kufanya lionekane ni tukio lenye sura ya kisiasa kuliko jinai.

Alisema ni mapema mno kulihusisha suala hilo na siasa na hawaelewi sababu za diwani huyo kukamatwa.

Hata hivyo, kamanda wa polisi wa mkoa, Salum Hamdani alisema hawajasema kama diwani huyo na wengine wamehusika bali wanashukiwa.

“Jukumu letu ni kuchunguza na kuwapata watu wote waliohusika kwa namna moja ama nyingine na kuchoma hiyo ofisi. Suala la mtu kukamatwa halina limitation (mipaka),” alisema Hamdani.

“Sisi tumekamata watu kadhaa ambao tunawashuku kuwa huenda wamejihusisha kwa namna moja ama nyingine na tukio hilo. Hatujasema wamehusika. Tunawatuhumu kuwa wamehusika,” alisema.

“Tunaendelea na taratibu za mahojiano na watapewa haki zao za msingi kulingana na sheria. Tunaendelea na upelelezi ila kuna watu kadhaa tunawashikilia akiwamo huyo diwani,” alisema.

Tukio lilivyokuwa
Taarifa iliyotolewa jana na Shaban Pazi kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa (RAS), inasema usiku wa kumkia jana, jirani anayeishi karibu na ofisi hiyo alihisi harufu ya moshi.

“Harufu ya moshi iliyochanganyika na mafuta ya petroli ilimshitua mkazi mmoja anayeishi jirani na ofisi hiyo ambaye alichungulia nje na kuona jengo la ofisi ya kata likiungua,” alisema.

Via Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527