AWAOMBA RADHI MASHABIKI WA SIMBA KWA KUJIUA GESTI... ATAKA MAZISHI YAKE WATU WACHEZE MPIRA


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya Henry Mwaibambe

Dinna Maningo - Malunde1 blog Rorya
Mkazi wa kijiji cha Kowaki Wilayani Rorya mkoani Mara Juma Okora amewataka Mashabiki wa timu ya  Simba SC,ndugu na marafiki kumsamehe baada ya kufanya maamuzi ya kujinyonga kutokana na ugumu wa maisha.


Akizungumza na Waandishi wa Habari Kamanda wa Polisi Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya Henry Mwaibambe amesema kuwa marehemu alikutwa kwenye chumba cha kulala wageni akiwa amejinyonga kwa kutumia kamba huku akiwa ameacha karatasi yenye ujumbe mrefu wa maandishi.

"Polisi walifika wakakuta ameshakufa na alikuwa kaandika barua ndefu, awali tulidhani labda kauawa na mtu na akaandika ujumbe kwa kujifanya ni marehemu, lakini tulivyofatilia kwa undani kwa kuangalia mwandiko na kumbukumbu za maandishi ya nyuma aliyokuwa akiyaandika wakati wa uhai wake tukagundua mwandiko ni wake na ameandika mwenyewe",amesema Kamanda Mwaibambe.

Mwaibambe amesema barua hiyo iliyoandikwa na marehemu ambayo ujumbe wake ulijikita kuwaomba watu msamaha na kuwashauri vijana kutafuta mali kwa njia za halali na si za kishirikina kwa kile alichodai kuwa kajiua kutokana na ugumu wa maisha na amekuwa akitafuta mali kwa njia za kishirikina bila mafanikio.

Baadhi ya ujumbe uliosomwa na Kamanda ulieleza"Nawaomba Washabiki wa Simba mnisamehe kwa maauzi haya ugumu wa Maisha umenifanya nijinyonge,Mke wangu Helen naomba unisamehe kwa kukuacha na mzigo wa kulea watoto peke yako,mdogo wangu......naomba uwatunze wanangu,Babu samahani".

"Bodaboda mnisamehe,rafiki zangu akina......mnisamehe na ninawaomba vijana mtafute mali kwa njia za halali nimetafuta kwa njia za kishirikina lakini sijafanikiwa nilipewa masharti magumu yamenishinda nimeamua kujinyonga naomba siku ya mazishi yangu watu wacheze Mpira",alisema Mwaibambe

Hata hivyo Kamanda Mwaibambe amewataka wananchi kutochukua maamuzi ya kujiua huku akieleza kuwa ujumbe wa marehemu nifundisho kwa vijana nakwamba wanapaswa kuwa wavumivu katika Maisha .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527