WASICHANA 91 MSALALA WA JAMII ZA WAFUGAJI WALIONUSURIKA KUOLEWA WANUFAIKA NA ELIMU BURE


Happiness Julias akiweka kemikali katika kifaa cha maabara katika shule ya sekondari Segese.
Kwandu Mahita akichanganya kemikali katika maabara ya shule ya sekondari Segese.
Mtaalamu wa maabara Esta akiwaelekeza wanafunzi namba ya kufanya mazoezi kwa vitendo katika shule ya sekondari Segese.
Wanafunzi wakimsikiliza kwa makini Mwalimu wa sayansi katika maabara ya shule ya sekondari Segese jana hayupo pichani.
Wanafunzi wakimsikiliza kwa makini Mwalimu wa sayansi katika maabara ya shule ya sekondari segese jana hayupo pichani.


Na Salvatory Ntandu - Kahama

Wasichana 91 kati ya wanafunzi 113 wa jamii za Wafugaji waliohitimu darasa la saba mwaka huu katika shule za msingi zilizopo katika kata ya Segese katika halmashauri ya Msalala mkoa wa Shinyanga wameanza kujifunza kwa vitendo masomo ya sayansi ili kuwahamasisha kupenda masomo hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari mratibu darasa maalumu la elimu kwa wanafunzi wakike, Patrick Mahona amesema wamejipanga kikamilifu ili kuhakikisha wasichana hao wanapata haki yao ya msingi ya elimu baada ya kuwanuru wimbi la kuolewa pindi wanapomaliza elimu ya Msingi.

“Wafugaji katika kata ya Segese mwaka huu walipiga marufuku tabia za wazazi kuwaoza watoto wao pindi wanapohitimu darasa la saba kukubaliana kuanzisha darasa maalumu kwa wasichana 90 ili wajifunze masomo ya awali ya kujiandaa na elimu ya sekondari”,alisema Mahona.

Mahona amesema katika jamii hizo ndoa za utotoni zimekuwa zikishamiri pindi watoto wakike wamapohitimu elimu ya msingi kutokana na wengi wao kutowathamini watoto wa kike hali ambayo imekuwa ikisababisha kushindwa kupata elimu kutokana na kuolewa hata kama watakuwa wamefaulu kuendelea na masomo.

Nao baadhi ya Wanafunzi waliopata mafunzo katika darasa hilo Happness Julius na Kwandu Mashita wamewapongeza wadau wa elimu katika kata hiyo kwa kutambua umuhimu wa mtoto wa kike katika masomo hasa kwa kundi la wafugaji.

“Tangu darasa hilo lilipofunguliwa tumejifunza masomo yote ambayo yatatusaidia kujiandaa na masomo ya sekondari hapo mwakani ambapo mpaka sasa tumeweza kuingia katika maabara za sayansi na kujifunza kwa vitendo majaribio mbalimbali",alisema.

Kwa upande Mwalimu Jeconia Mlinda kutoka shule ya sekondari Segese amesema wanafunzi hao wamejifunza masomo yote kwa nadharia na vitendo ambayo yatawasidia kufanya vizuri katika masomo yao hususani ya sayansi.

“Niwaombe wazazi kuwahamsisha watoto wenu kujifunza masomo ya sayansi kwani yatawasidia kukabiliana na wimbi la ajira wataalamu wa sayansi wanahitajika sana katika kada mbalimbali hususani sekta ya afya”,alisema Mlinda.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527