UMOJA WA MATAIFA WAIPONGEZA TANZANIA KWA ULINZI WA AMANI UKANDA WA MAZIWA MAKUU

Na Mwandishi Wetu,

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Dkt. Amina Mohammed ameisihi Tanzania kuendelea kuimarisha amani katika ukanda wa maziwa makuu pamoja na kuendelea kuchangia kutoa askari wa vikosi vya ulinzi wa amani duniani.

Naibu Katibu Mkuu Dkt. Amina Mohammed ametoa wito huo alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiorikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) Jijini New York nchini Marekani na kuongeza kuwa Umoja wa Mataifa unatambua mchango wa Tanzania katika ulinzi wa amani duniani na kwamba Umoja huo uko tayari kushirikiana na Tanzania katika kuendeleza jitihada hizo ili kuifanya dunia kuwa sehemu salama ya kuishi.

“Tanzania imekuwa muhimili muhimu katika kuhimiza amani katika ukanda wa maziwa makuu ikiwa ni pamoja na kuhifadhi wakimbizi kutoka ukanda huo kwa miaka mingi bila kuchoka” alisema Dkt. Amina

Kwa upande wake waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi amesema kuwa Tanzania inatambua nafasi ya Umoja wa Mataifa na kwamba itasalia kuwa mwanachama wa umoja huo.

“Napenda kukuhakikishia kuwa Tanzania itaendelea kutoa askari wake katika vikosi vya ulinzi wa amani katika maeneo mbalimbali duniani,” alisema Prof. Kabudi

Waziri Kabudi aliendelea kumueleza Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa hatua mbalimbali ambazo Tanzania imepiga katika masuala ya maendeleo endelevu (SDGs) ikiwa ni pamoja na afya,maji, ushirikishwaji wa wanawake katika maamuzi pamoja na masuala ya kuimarika kwa demokrasia nchini.

Prof. Kabudi amehitimisha ziara yake ya kikazi nchini Marekani alipokuwa akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli katika Mkutano wa 74 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527