TAKUKURU SHINYANGA YAWAONYA WAGOMBEA KUENDEKEZA RUSHWA KWENYE UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA


Kaimu Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Shinyanga Hussein Mzee Mussa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu mikakati mbalimbali ya TAKUKURU kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa Novemba 24 mwaka huu. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Shinyanga imetoa onyo kwa wagombea wote katika uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba 24,2019 kutojihusisha na vitendo vya rushwa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano Oktoba 9,2019, Kaimu Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Shinyanga Hussein Mzee Mussa amesema ni vyema wagombea wote katika uchaguzi kuwa makini na mienendo yao na kuhakikisha kwa namna yoyote hawajihusishi na vitendo vya rushwa.

"Wagombea wote wawe makini na vitendo vyovyote kinyume na sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa Na.11 ya mwaka 2007 pamoja na sheria ya gharama za uchaguzi kama zilivyoanishwa na sheria ya gharama za uchaguzi Na. 6 ya mwaka 2010",amesema Mussa.

Amebainisha kuwa mikakati ya TAKUKURU kuelekea kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa ni kutoa elimu ya rushwa kwa njia ya mikutano ya hadhara,semina mbalimbali na kupitia vyombo vya habari.

"Tunatoa elimu ya rushwa kwa wananchi wote wakiwemo wapiga kura na watakaogombea nafasi za uongozi. Elimu hii inahusu athari za rushwa kwenye uchaguzi,makosa ya rushwa katika uchaguzi kisiasa,sheria ya gharama za uchaguzi kama zilivyoainishwa na sheria ya gharama za uchaguzi Na. 6 ya mwaka 2010 na makosa yaliyo kwenye sheria ya Kuzuia na kupambana na rushwa Na. 11 ya mwaka 2007",ameeleza Mussa.

"Nitoe wito kwa wananchi waendelee kutoa ushirikiano kwa TAKUKURU ili kuhakikisha kuwa tunaondoa kero ya rushwa hasa katika kipindi hiki tunachoelekea kuanza michakato ya uteuzi wa wagombea wa uongozi wa serikali za mitaa",ameongeza Mussa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527