RAIS MAGUFULI AONGOZA MAELFU YA WATANZANIA KUPOKEA NDEGE MPYA YA SERIKALI YA BOEING 787-8 DREAMLINER

Na Mwandishi Wetu,MAELEZO
RAIS Dkt. John Magufuli amesema Tanzania itaendelea kutekeleza kwa kasi kubwa miradi ya maendeleo nchini kwa kuwa Serikali imeimarisha nidhamu katika usimamizi na matumizi ya rasilimali zilizopo pamoja na ukusanyaji wa kodi.


Akizungumza katika hafla ya upokeaji wa ndege mpya ya Serikali ya Boeing 787-8 Dreamliner katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo Jumamosi (Oktoba 26, 2019) Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli aliwataka Watanzania kujivunia na kuendelea kuiunga mkono Serikali yao kwa kuwa imedhamiria kuwaletea maendeleo ya kweli na ya haraka.

Rais Magufuli alisema Tanzania na Bara la Afrika kwa ujumla lina uwezo wa kufanya mambo makubwa  nay a haraka kutokana na kubarikiwa na rasilimali nyingi ikiwemo madini na hivyo Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kusimamia rasilimali hizo ili ziweze kuleta manufaa yaliyokusudiwa kwa wananchi walio wengi.

‘’Watanzania sisi ni matajiri tunaweza kufanya mambo makubwa na kununua vitu vizito kama ndege hizi, na tukiamua tunaweza kinachotakiwa sasa ni kuweza kuwa na matumizi mazuri ya fedha zinazopatikana kutokana na kodi tunazokusanya kutoka kwa wananchi wetu’’ alisema Rais Magufuli.

Aliongeza kuwa malengo ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kuwa sekta ya usafiri wa anga inapiga hatua kubwa ya maendeleo nchini na kwa kufanya hivyo Serikali imekusudia kuliwezesha Shirika la Ndege Nchini ATCL kuweza kutekeleza mipango na mikakati mbalimbali iliyojiwekea.

Akifafanua zaidi Rais Magufuli alisema ATCL kwa sasa ina jumla ya ndege 7 kati ya ndege 11 zilizopangwa kununuliwa na Serikali, hivyo aliitaka Menejimenti ya Shirika hilo kujipanga vizuri ili kuhakikisha kuwa linamudu ushindani wa kibiashara uliopo nchini ikiwemo kuimarisha mtandao wa usafirishaji abiria katika soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Rais Magufuli alisema ndege hiyo mpya ya Boeing 787-8 Dreamliner ni ndege kubwa ya kisasa yenye uwezo wa kubeba abiria 262 ikiwemo abiria 22 wa daraja la juu pamoja abiria 240 katika daraja la kawaida, hivyo kuitaka ATCL kuweka mipango na mikakati endelevu ya kuhakikisha itangaza vyema vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

‘ATCL hamna budi kujiendesha kibiashara na mnapaswa kutambua ndege hii ni mali ya Serikali na si ya ATCL hivyo na hilo linajionesha katika mkataba tuliosaini baina ya Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu Mkuu (Uchukuzi), hivyo hakikisheni mnafikia malengo yote tuliyowekeana’’ alisema Rais Magufuli.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Dkt. Leonard Chamuriho alisema Shirika la ATCL limeendelea kutekeleza kwa mafanikio makubwa Mpango Mkakati wa Shirika hilo, ambapo sasa limeweza kufikia mafanikio ya asilimia 73 la usafirishaji wa abiria katika soko la ndani.

Aidha Dkt. Chamuriho anaongeza kuwa kutokana na kuongezeka kwa idadi ya safari za abiria nje ya nchi, Shirika hilo pia limefanikiwa kuongeza idadi ya upokeaji wa shehena za mizigo kutoka nchini India na kufikia tani 178 na kuzisafirisha katika nchi mbalimbali ikiwemo Zambia.

Aliongeza kuwa Shirika hilo limepanga kushirikiana na Taaasisi ya Sekta Binafsi Nchini (TPSF) pamoja na Chemba ya Biashara,Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) kwa ajili ya kuweka nguvu na mkakati wa pamoja wa kuhakikisha kuwa inatanua mtandao wa usafirishaji wa shehena za mizigo nchini India.

Kuhusu soko la ndani, Dkt.Chamuriho aliongeza kuwa Shirika hilo limeweza kuongeza kituo cha usafirishaji wa abiria katika Kituo cha Mpanda Mkoani Rukwa pamoja na kupanga kuongeza idadi ya miruko ya ddege kutoka Dar es Salaam-Dodoma kufikia mara nne kwa siku ifikapo mwezi Desemba mwaka huu.

Naye Kaimu Balozi wa Marekani Nchini , Dkt. Imni Patterson aliipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kutokana na juhudi na hatua mbalimbali za makusudi inazochukua katika kuimarisha sekta ya usafiri wa anga kwani kwa kufanya hivyo kutaweza kutangaza sekta ya utalii pamoja na kuimarisha uchumi.

MWISHO



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527