KURA ZA MAONI CCM ZAFUTWA MAENEO YENYE MALALAMIKO, VURUGU


Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Bashiru Ally, amesema chama hicho kumeamuru kufutwa kwa kura ya maoni maeneo yote ambayo yalikuwa na ukiukwaji wa kanuni, kisha kurudiwa upya.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Dk. Bashiru alisema kura hizo zitarudiwa bila kujali kanuni kwa kuwa zilikiukwa katika maeneo yote yanayolalamikiwa.

Alisema wote waliokuwa wamechukua fomu sasa watapata fursa ya kuchujwa kupitia kura za wanachama na si kamati za uongozi.

Dk. Bashiru alisema kutokana na hitilafu hizo, katika maeneo yote ambayo uongozi wa chama umeorodhesha na unaendelea kuorodhesha hitilafu, upigaji kura utarudiwa tena bila kufuata utaratibu wa mchujo, kama ilivyokuwa awali.

Alisema kwa sasa wale wote waliokuwa wamechukua fomu awali watapigiwa kura na mchujo wao utafanywa kwa kura za wanachama, bila kujali idadi ya waliokuwa wamechukua fomu.

“Na kwa sasa tumeamua kufanya hivi si kwa nia ya kukiuka kanuni na taratibu, bali kwa kuwa hakuna muda wa kutosha kuanza mchakato huo upya.

“Wakati wote tumekuwa tukisisitiza utii wa katiba, kanuni na taratibu za chama. Tumekuwa tukisisitiza tusipuuze maelekezo ya chama na Serikali,” alisema.

Dk. Bashiru alifafanua kuwa ni katika utaratibu huo, uongozi umeamua kuongeza siku mbili zaidi katika mchakato wa ndani ya chama, kutoka Oktoba 29 hadi Oktoba 31 ili kukamilisha marudio hayo.

“Kwa kuwa utaratibu wa wagombea wa vyama kuchukua fomu kule serikalini unaanza Oktoba 29 hadi Novemba 4, ninaamini tutawahi kukamilisha na wagombea wetu watachukua fomu kwa wakati,” alisema.

Alisema yapo maeneo ambayo hayakuzingatia kanuni za chama katika kuteua, yapo ambayo hapakuwa na maelewano katika uteuzi na yapo ambayo hayakufuata utaratibu wa uteuzi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527