ASILIMIA 68 WAJIANDIKISHA KUPIGA KURA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA


Watanzania 15,543,604 sawa na asilimia 68 wameshajiandikisha kwenye daftari la wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali unaotarajiwa kufanyika Novemba 24 mwaka huu.


Aidha, Mkoa wa Pwani umeongoza kwa kundikisha watu 473,639 sawa na asilimia 80, mkoa wa Dar es Salaam uliondikisha watu 2,064,820 sawa na asilimia 77 na Tanga ulioandikisha watu 823,194 sawa na asilimia 76.

Mikoa mingine ni Mtwara watu 530,523, Lindi watu 353,649 sawa na asilimia 75 na Iringa watu 381,134 sawa na asilimia 74.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo, ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam, wakati akielezea tathimini ya uandikishaji ulioanza Octoba 8 hadi 14.

"Tamisemi imejiwekea malengo ya kuandikisha wapiga kura watapatao milioni 22.916 wenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu, baada ya hamasa iliyofanywa na wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya watendaji idadi ya waliojiandikisha imefika watu milioni 15.543 sawa na asilimia 68 ya lengo," Jafo amesema

Aidha, amesema mikoa ambayo ipo chini kiuandikishaji hadi juzi ni Kilimanjaro ambayo imeandikisha watu 446,954 sawa na asilimia 48, Kigoma watu 555,856 sawa na asilimia 53 na Arusha watu 551,614 sawa na asilimia 59.

Amesema pia zipo Halmashauri sita ambazo zimefanya vizuri zaidi kwa kuandikisha zaidi ya asilimia 95 na kuendelea ambazo ni Mpanda, Mlele, Kibiti, Ngorongoro, Songwe na Mbozi.

Jafo amezitaja pia Halmashauri ambazo zimeandikisha chini ya asilimia 50 ambazo Manispaa za Moshi kwa asilimia 31, Jiji la Arusha kwa asilimia 32, Msimbo asilimia 41, Kigoma asilimia 43, Jiji la Mbeya asilimia 46 na Musoma asilimia 49.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527