WAZIRI WA AFYA: HAKUNA UGONJWA WA EBOLA TANZANIA


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amewatoa wasiwasi Watanzania juu ya uvumi wa uwepo wa Ebola Nchini Tanzania ambapo amesema mpaka sasa hakuna yeyote aliyethibitishwa kuwa na Ebola hapa Nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi Septemba 14, 2019 Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akiwa na naibu wake, Dk Faustine Ndugulile, mganga mkuu wa Serikali, Profesa Mohamed Kambi na jopo la wataalam  wa Shirika la Afya Duniani (WHO), amewataka wananchi kutokuwa na hofu yoyote.

Amebainisha kuwa taarifa za kuwepo kwa ugonjwa huo nchini zimetokana na watu wawili kudhaniwa kuwa na maambukizi ya Ebola katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.

“Hawa walikuwa wahisiwa lakini wizara imefanya vipimo vya maabara zaidi ya mara moja kama inavyoelekezwa na mwongozo wa WHO na kujiridhisha kwamba hawakuwa  na maambukizi ya virusi vya ebola hivyo hakuna ugonjwa huo Tanzania,” amesema Waziri Ummy


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527