WAZIRI MKUU : SADC TUWEKE SERA NA VIWANGO VYA AINA MOJA KURAHISISHA USAFIRISHAJI WA BIDHAA NAUKUZAJI BIASHARA

Na Mwandishi Wetu,MAELEZO

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amezitaka Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuwa kuwa na mipango, sera, viwango na mifumo ya pamoja ya kisheria itakayorahisha utoaji wa huduma za usafirishaji wa bidhaa na kukuza biashara ndani ya Ukanda huo.


Akifungua Mkutano wa Mawaziri wa Jumuiya hiyo wanaosimamia sekta za Tehama, Habari, Uchukuzi na Hali ya Hewa jana Alhamisi (Septemba 19, 2019) Waziri Mkuu Majaliwa aliwataka Mawaziri hao kutumia mkutano kuandaa mapendekezo ya suluhisho la changamoto ya nnjia bora za kuimarisha mtandao wa biashara ndani ya sadc.

Majaliwa alisema Tanzania kwa upande wake imekuwa mstari wa mbele katika nja wanachama wa SADC katika kuboresha miundombinu ya usafirishaji ikiwemo kuboresha bandari ya Dar es Salaam ambayo kwa sasa imekuwa ikihudumia  Nchi mbalimbali za Jumuiya ya SADC ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya  Kongo, Malawi na Zambia pamoja na Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aliongeza kuwa Tanzania pia imeendelea na ujenzi na reli ya kisasa inayojengwa katika Ukanda wa kati pamoja na ujenzi wa reli ya Tazara inayonganisha Tanzania na  Zambia, na kutaja juhudi hizo ni moja ya mikakati ya Tanzania ya kuhakikisha inaimarisha mtandao wa biashara ndani ya Jumuiya hiyo.

“Katika Ukanda wa reli ya Tazara kwa sasa tumeweza kuongeza kiwango cha usafirishaji kutoka tani 88,000 mwaka 2014/2015 hadi kufikia tani 220,000 mwaka 2017/2018 pamoja pia na kujenga Meli 2 za mizigo katika Ziwa Nyasa zenye uwezo wa kubeba tani 200” alisema Majaliwa

Akizungumzia kuhusu Maendeleo ya Sekta ya Tehama katika Ukanda wa SADC, Majaliwa alisema Nchi hizo hazina budi kufikia malengo yaliyowekwa katika Mkutano Windohoek Nchini Namibia mwaka 2018 wa kuhakikisha kuwa kunawepo na Intaneti yenye kasi kwa ajili ya kurahisisha shughuli za kibiashara na utoaji huduma kwa wananchi ifikapo mwaka 2023.

Aliongeza kuwa kwa mujibu wa taarifa ya  Shirika la Mawasiliano  Duniani (ITU) zinaonesha kuwa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasliano katika Nchi za SADC imekuwa na kufikia asiliami 22.3 ikilinganisha na kiwango cha dunia ambacho ni asilimia 51, na hivyo kuwa katika kiwango cha juu ikilinganishwa na kiwango kilichowepo katika miaka ya 2000.

Akifafanua zaidi Waziri Mkuu Majaliwa aliwataka Mawaziri hao kuweka mkazo katika kujadili kiwango cha matumizi na umuhimu wa kuunganisha Intaneti ili kuweza kuongeza kasi ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa Jumuiya hiyo.

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe alisema kutokana na Nchi za SADC kuwa na changamoto zinazoshabihiana katika masuala ya hali ya hewa, Tehama, Uchukuzi na Habari, Mkutano wa Mawaziri hao umepanga kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha ustawi wa wananchi wake.

Aidha aliongeza kuwa Mkutano huo umehudhuriwa na Mawaziri wa Nchi 8 za Jumuiya hiyo ikiwemo Angola, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini, Lesotho, Zimbambwe, Tanzania ambapo Mawaziri hao katika Mkutano wao wa siku mbili wanatarajia kujadili masuala mbalimbali ikiwemo maazimio yaliyopitishwa katika Mkutano Mkuu wa 39 wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya hiyo uliofanyika Agosti 17-18 mwaka huu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miundombinu na Huduma wa SADC, Rosemary Mokoena alisema Mkutano huo wa Mawaziri unatarajia kujadili masuala mbalimbali ambayo ni muhimu katika utekelezaji wa Mipango Mkakati mbalimbali iliyopangwa kutekelezwa na jumuiya hiyo katika kuimarisha mifumo ya biashara na huduma mbalimbali ndani ya SADC.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527