WAZIRI MKUU AWASIMAMISHA KAZI WATUMISHI SABA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewasimamisha kazi watumishi saba katika halmashauri mbili za wilaya ya Kilombero na  kwa tuhuma za ubadhilifu wa fedha zaidi ya sh. bilioni 1.3 za makusanyo ya mapato ya ndani.


Mbali na kuwasimamisha kazi watumishi hao, pia Waziri Mkuu ameagiza watumishi hao warejeshe fedha hizo ndani ya siku tatu kabla hajamaliza ziara yake ya kikazi mkoani Morogoro. Watumishi hao ni pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Ifakara  Fransis Ndulane anayedaiwa  sh. milioni tano alizoingiziwa katika akaunti yake bila maelezo yeyote.

Waziri Mkuu amewasimamisha kazi watumishi ha oleo (Jumapili, Septemba 15, 2019) wakati akiongea na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara, akiwa katika siku ya pili za ziara yake ya kikazi mkoani Morogoro.

Amesema “Mkoa mzima wa Morogoro umekuwa na tatizo la upotevu wa mapato, fedha zinakusanywa zinapita mikononi mwa watu hazifiki benki, hii ni shida, hatutavumilia.”

Waziri Mkuu amesema kwa mujibu wa taarifa ya mkaguzi wa hesabu za serikali (CAG) kipindi cha mwaka 2016 hadi juni 2019, Katika mji wa Ifakara  makusanyo yalikuwa ni bilioni 2.7  ambapo fedha iliopelekwa bank ni shilingi bilioni 1.9   na kwamba kiasi cha  shilingi milioni 727  hazijulikani zilipoenda.

Amesema katika mitambo kumi  ya ukusanyaji wa mapato iliokaguliwa imeonyesha kiasi cha shilingi milioni 348 zilizokusanywa hazikupelekwa bank na hivyo kuishia mikononi mwa watu.

Waziri Mkuu amesema katika uchunguzi huo ilibainika kuwa fedha hizo ziliingizwa katika akaunti mbalimbali za watumishi wa halamshauri hizo  kutoka kwa mtendaji wa Kata ya Viwanja 60 katika Mji wa Ifakara aitwaye Gregory Midas.

Watumishi   hao ni  Reina Mrema ambaye anadaiwa kuchukua kiasi cha shilingi 298, Haile Njitango milioni 73 , Linus Mdembo kiasi cha shilingi milioni 2 kwa kushirikiana na mtendaji huyo wa Kata.

Hata hivyo Waziri Mkuu ameagiza Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA katika halmashauri ya Mji wa Ifakara, John Mvanga ambaye ndiye alibaini kuwepo na ubadhilifu wa fedha hizo na badae kusimamishwa kazi, arejeshwe kazini mara moja na asibugudhiwe.

“Mlimsimamisha kazi  kwa sababu mlijua amegundua madudu yenu, lakini haisaidi, arejeshwe kazini naagiza apewe ulizi  wakutosha.”

Kwa upande wa Halmashauri ya wilaya ya Kilombero, Waziri Mkuu amesema  zaidi ya sh. milioni 600 hazijulikani zilipo huku  kiasi cha shilingi milioni 98.5 zikidaiwa kuingizwa katika akaunti za watumishi wa halamshauri hiyo bila maelezo yeyote.

Waziri Mkuu amewataja watumishi hao kuwa ni Devid Onyango aliyechukua kiasi cha milioni 51, Elakada Kanongole milioni 36, Fork Karunde milioni 8 na Charlse Chali milioni 2.5.Amesema kati ya milioni hizo 600 kampuni ya Kilombero Plantation LTD (KPL) ambao wanadaiwa kiasi cha shilingi milioni 531  ambazo hazikuingizwa katika mfumo huo.

(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527