SERIKALI YATAHADHARISHA WANANCHI KUPUUZA VITU VINAVYONG’ARA WASIOKOTE MABOMU


Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Hussein Mwinyi amewataka wananchi hususani mkoani Kagera, kuendelea kuchukua tahadhari ya kuokota vitu vinavyong’ara au vyuma wasije wakaokota mabomu.

Dk. Mwinyi amesema hayo akijibu swali la Mbunge wa Nungwi, Yussuf Haji Khamis, bungeni jijini Dodoma jana Jumanne Septemba 10, aliyeuliza mpango wa serikali katika kukomesha matukio ya watoto kuokota mabomu wakidhani ni vyuma chakavu na kusababisha madhara makubwa ikiwamo vifo.

“Hivi karibuni watoto watano wamepoteza maisha na zaidi ya watoto 40 kujeruhiwa katika Shule ya Msingi ya Kihinga iliyoko Ngara mkoani Kagera, je, serikali ina mpango gani wa kudhibiti na kukomesha tatizo hilo,” alihoji.

Akijibu swali hilo, Dk. Mwinyi alisema maeneo mengi duniani yanakabiliwa na kutapakaa kwa silaha ndogo ndogo yakiwamo mabomu ya kutupwa kwa mkono, Tanzania ni nchi yenye amani lakini baadhi ya nchi zinazotuzunguka zimejikuta zikiingia kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe.

“Hali hiyo imesababisha baadhi ya wakimbizi kukimbia na baadhi ya mabomu ya kutupwa kwa mkono na kuyatelekeza baada ya kujiona wako salama au kuwazuia wahalifu jambo ambalo limechangia kuwepo kwa mabonu hayo katika Mkoa wa Kagera.

“Baada ya vita ya Kagera Jeshi la Polisi lilitoa elimu kwa wananchi kutookota vitu vinavyong’ara au vifaa vya chuma na pindi wanapoona vitu hivyo watoe taarifa polisi au kwenye kambi ya jeshi iliyo karibu.

“Kwa maeneo yaliyotolewa taarifa wananchi walitaarifiwa kutopita, kulima au kulisha mifugo. Aidha, Jeshi la Wananchi lilipeleka wanajeshi wa medani kujiridhisha kama maeneo hayo yako salama kwa wananchi kuendelea na shughuli zao za kawaida.

“Hata hivyo, wanashauriwa wananchi katika maeno hayo kuendelea kuchukua tahadhari ya vitu hivyo,” alisema Dk. Mwinyi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527