SERIKALI YAINGILIA KATI NAMBA ZA UTAMBULISHO WA URAIA ....YAONESHA KUTORIDHIKA NA KASI, WAZIRI MKUU ATOA MAAGIZO KWA NIDA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameitaka Mamlaka  ya Usajili wa Vitambulisho vya Taifa  (NIDA) ihakikishe wananchi  hasa walioko vijijini wanapata angalau  namba za utambulisho wa usajili wao kabla ya muda wa usajili wa laini za simu haujamalizika.


Ametoa agizo hilo jana (Jumamosi, Septemba 21, 2019) wakati alizungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa hospitali ya wilaya ya Geita iliyopo kwenye Kijiji cha Nzela.

Alisema kitendo cha kuwapatia namba za utambulisho wa usajili wananchi ambao hawajapata vitambulisho vya uraia kitawezesha kuingia kwenye orodha ya wale wanosubiri kusajiliwa hata kama muda wa usajili utakuwa umeisha. Mwisho wa muda wa usajili ni Desemba mwaka huu.

Waziri Mkuu alisema Serikali imewapatia NIDA vifaa vya kisasa vya kielektroniki ili wafanye kazi zao kwa haraka na ufanisi, lakini hali hairidhishi kwa sababu wananchi wengo bado hawajapata vitambulisho na kasi ya usajili wa laini za simu inalalamikiwa katika meneo mengi.

“NIDA mnalalamikiwa, nimeenda Morogoro Vijijini NIDA mnalalamikiwa hivi utendaji wenu uko je? Kwanini mnachelewa ?” Waziri Mkuu alimuuliza Afisa Msajili wa NIDA wa wilaya ya Geita, Paschal Saro ambaye  alijitetea kwamba wamesajili laini za simu 340 na tayari namba za usajili 330 zimeshatolewa.

Saro alimwambia Waziri Mkuu kuwa suala la utata wa uraia kwa baadhi ya wananachi wanaoomba vitambulisho vya NIDA ni moja ya sababu zinazochelewesha  usajili wa vitambulisho vya uraia.

Waziri Mkuu aliwasihi wananchi wote kuwa walinzi wa nchi yao kwa kutoa taarifa za watu ambao wanaomba viutambulisho vya uraia wa Tanzania wakati si raia na aliwataka watoe taarifa mara moja kwenye vyombo vya dola pale wanapogundua kuwa kuna raia wa nje anafanya mchakato wa kuapata vitambulisho hivyo.

Alisema katika baadhi ya mikoa ya mipakani ambayo ina wakimbizi Serikali imekamata silaha ambazo raia hawasurusiwi kuzimiliki na zinasadikiwa kuwa zimepenyezwa nchini na raia wa nje wasiowaaminifu.

Awali,Waziri Mkuu, alikagua ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Geita iliyopo katika kijiji cha Nzera mkoani Geita na kufurahishwa na hatua ya Mbunge wa jimbo wa Geita Vijijini, Joseph Musukuma ambaye amewezesha upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa kwa ajili ya hospitali hiyo.

Waziri Mkuu alimpongeza Musukuma kwa moyo wa upendo alionao kwa  wapiga kura wake.  Vifaa hivyo ni vya kisasa na vinastahili kuwa katika hospitali za rufaa za mikoa lakini mbunge huyo ameamua kuwapelekea wapiga kura wake kwenye hospitali ya wilaya lengo likiwa ni kuboresha huduma.

(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527