Makubwa Haya : MREMBO AZIMIA AKIOMBA PENZI LA MUME WA MTU

NANI kasema wanawake hawawezi kuwatongoza wanaume? Mjini Morogoro mwanamke mmoja (jina halikupatikana) amejikuta akizimia wakati akimuomba penzi mume wa mtu. 

Tukio hilo la aina yake limetokea mwishoni mwa wiki iliyopita mchana kweupe eneo la Lunna karibu na soko kuu tena kwenye mkusanyiko wa watu wengi.
Awali macho ya mashuhuda yalimwona mwanamke huyo ambaye alitajwa pia kuwa ni mwanafunzi wa chuo (jina linafichwa) akifika Barabara ya Makongoro mahali anapouzia viungo vya mboga kijana mmoja ajulikanaye kwa jina la Mwanakwetu akidhaniwa kuwa ni mteja. Walichomuwazia watu haikuwa haja ya mwanamke huyo kwa Mwanakwetu bali alifika hapo kwa lengo la kumfikishia hisia zake kuwa anampenda kinomanoma.

“Alipofika alinikuta nikiwa na mke wangu eneo la biashara, nadhani hamfahamu, nilipomkaribisha kibiashara akaanza kuniambia kuwa ananipenda tangu siku nyingi na kwamba alikuwa anahitaji tuwe wapenzi.

“Mimi nikabaki namshangaa; kwanza kwa yeye kunitamkia maneno hayo mbele ya mke wangu lakini pia katika maisha yangu sijawahi kuona mwanamke anamtongoza mwanaume,” alisema Mwanakwetu.

Aliongeza kuwa, mshangao wake haukumzuia mwanamke huyo kuendelea kupanga mistari ya kumuweka sawa jambo lililomfanya Mwanakwetu amtamkie wazi kuwa jambo hilo haliwezekani. “Alisema maneno mengi kwamba amekuwa akifika mara kwa mara kwenye biashara yangu kununua nyanya na vitunguu na kwamba kwa muda mrefu amekuwa akinipenda lakini alikuwa anashindwa kuniambia.
“Mwanamke mwenyewe alionekana kama amelewa, nikamuuliza akasema ameamua kunywa pombe aondoe aibu ili aweze kunifikishia hisia zake,” alisema. Aliongeza kuwa, wakati akiendelea kumkatalia ombi lake mwanamke huyo ghafla alidondoka chini na kupoteza fahamu.

Tukio hilo lilikusanya watu wengi akiwemo mwandishi wetu ambaye alifika na kuanza kuchukua picha na baadaye kufanya mahojiano na Mwanakwetu. Aidha, baadhi ya watu walimchukua mwanamke huyo na kumpeleka hospitalini kwa ajili ya kupatiwa tiba huku nyuma akiacha gumzo la aina yake.
Wakati hayo yakiendelea, mke wa Mwanakwetu aitwaye Grace alikuwa bado hajaelewa picha ilivyokuwa ikiendelea lakini baadaye aligeuka mbogo na kutaka kujua mumewe amefahamiana vipi na huyo mwanamke?

Ingawa alipewa jibu na mumewe kuwa hamfahamu huyo mwanamke lakini bado mkewe aliendelea kubwata hadi pale alipokuja kutulizwa na mzee mmoja aitwaye Abdul Mrisho ambaye ni fundi maarufu wa baiskeli eneo hilo.

STORI: DUNSTAN SHEKIDELE, RISASI MCHANGANYIKO

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527